KATIBU
TAWALA BAGAMOYO AKERWA NA ‘WIZI’ WA DAWA
NA
VICTOR MASANGU, BAGAMOYO
SERIKALI wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani, imekemea vikali tabia
ya baadhi ya watumishi wa afya kuamua kukiuka viapo vya kazi zao
kwa kujihusisha na vitendo vya wizi wa madawa na kutoa lugha chafu kwa wagonjwa
hali ambayo ni kinyume kabisa na maadili ya utekelezaji wa
majukumu yao.
Kauli hiyo, imetolewa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Bagamoyo,
Kasilda Mgeni wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kutembelea katika
kituo cha afya Kerege kwa ajili ya kuweza kujionea huduma mbali mbali
zinazotolewa na watumishi hao wa afya pamoja na kusikiliza changamoto
zilizopo kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi.
“Nimeweza kutembelea katika kituo hiki cha afya Kerege niweze
kuzungumza na watumishi mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuweza kujionea shughuli
mbali mbali ambazo zinafanyika ikiwa ni kuona namna ya kuweza kuboresha sekta
ya afya ili wananchi waweze kupata fursa ya kupata matibabu yanayostahili na hii
itapunguza kwa kiwango kikubwa malalamiko ya wananchi,”alisema Mgeni.
Aidha, Mgeni aliongeza kuwa, lengo la serikali ya awamu ya tano
ni kuhakikisha kwamba inaendelea kuboresha huduma ya afya kwa wananchi na
kuwaondolea changamoto mbali mbali zinazowakabili kwa kuweka mipango madhubuti
ya kuongeza wataalamu zaidi wa afya ikiwemo kujenga zahanati, vituo vya afya
pamoja na hospitali lengo ikiwa ni kuboresha zaidi huduma ya matibabu kwa
wananchi.
Pia,Katibu huyo, alisema kuwa,ameakua kufanya ziara zake za kikazi
katika maeneo mbali mbali ya zahanati, vituo vya afya pamoja na Hospitali
katika Wilaya hiyo ambayo itaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kuibua changamoto
mbali mbali ambazo zinawakabili wauguzi, madaktari pamoja na watumishi
wa afya na kuzisikiliza changamoto
ili kuzifanyia kazi.
Katibu Tawala huyo, alisema kwamba inasikitisha sana kuona Rais wa awamu ya Tano Dk. John Pombe Magufuli akitoa fedha nyingi kwa ajili kuboresha huduma katika sekta ya afya lakini bado kunakuwepo na baadhi ya wananchi kutoa malalamiko juu ya upatikanaji wa huduma ya afya.
Kadhalika, alibanisha kuwa malalamiko mengi ambayo yanatolewa
na baadhi ya wananchi ni kuwepo kwa kucheleweshewa huduma ya matibabu
kutokana na baadhi ya watumishi kuomba rushwa na wengine kuwa na lugha ambayo
sio rafiki na kutoa huduma kwa upendeleo hali hiyo ambayo inapelekea kuibuka
kwa malalamiko hayo.
Katika hatua nyingine, amesikitishwa na tatizo la wizi wa madawa katika vituo hivyo vya afya ambapo amedai kumekuwa na baadhi ya watumishi kuamua kuiba madawa na kwenda kuyauza katika maduka yao binafsi kinyume kabisa na sheria na taratibu za nchi na kupeleeka ukosefu wa madawa kwa wananchi hao.

No comments:
Post a Comment