Breaking News

Jan 30, 2026

TAKUKURU YAGAWA VIFAA TIBA, KUOKOA MAISHA YA WATOTO NJITI

 


TAKUKURU YAGAWA VIFAA TIBA KUOKOA MAISHA YA WATOTO NJITI  MOROGORO

Na Thadei Hafigwa

KUTOKANA na changamoto zinazoikabili sekta ya afya nchini, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeazimia kufanya matendo ya huruma kwa kugawa vifaa tiba vya kisasa kwa ajili ya kusaidia watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya wakati (watoto njiti) katika hospitali zote za rufaa nchini.

Hatua hiyo ilidhihirishwa mjini Morogoro wakati wa hafla ya kukabidhi mashine mbili za Phototherapy na Neonatal Radiant Warmer kwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, hafla iliyohudhuriwa na viongozi wa hospitali hiyo pamoja na maafisa wa TAKUKURU kutoka ngazi ya mkoa na taifa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Francis Chalamila, alisema msaada huo ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuboresha huduma za afya nchini, hususan huduma za mama na mtoto.


Chalamila alisema kuwa, menejimenti ya TAKUKURU ilifanya uamuzi huo kwa misingi ya utu, busara na hekima baada ya kubaini kuwa kuna uhitaji mkubwa wa vifaa tiba katika hospitali mbalimbali nchini, hususan vifaa vya kuwahudumia watoto njiti.

“Taarifa tulizozipata kutoka vituo vya kutolea huduma za afya zinaonesha kuwepo kwa uhitaji mkubwa wa vifaa tiba, hasa mashine za kuwasaidia watoto njiti ili kunusuru maisha yao,” alisema Chalamila.

Alifafanua zaidi kwamba, ununuzi wa mashine hizo umewezeshwa na michango ya hiari kutoka kwa watumishi wa TAKUKURU, waliotoa sehemu ya mishahara yao, akibainisha kuwa taasisi hiyo haina mfuko maalumu wa uwajibikaji kwa jamii kama ilivyo kwa baadhi ya taasisi nyingine.

“Tupo katika zoezi la kugawa mashine za kuwasaidia watoto njiti katika hospitali zote za rufaa nchini. Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ni hospitali ya kumi kufikiwa, na tunaendelea kufikia mikoa mingine hivi karibuni,” alisema Chalamila.


Kwa mujibu wa Mkurugenzi mkuu wa Takukuru, hatua hiyo ni matendo ya huruma na hiyari kwa watumishi wa TAKUKURU, ambao wameguswa na uhitaji mkubwa uliopo katika jamii, sambamba na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha huduma za afya nchini.

Naye, Kaimu Mratibu wa Huduma za Tiba wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk. Azael Haward Kyando, alisema hospitali hiyo hupokea mara kwa mara idadi ya watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati, wakiwemo wenye uzito mdogo na wanaohitaji uangalizi wa karibu mara tu baada ya kuzaliwa jambo linaloashiria uwepo mkubwa wa tatizo hilo.

 “Watoto njiti hukumbwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo kushindwa kudhibiti joto la mwili, hatari ya maambukizi, matatizo ya kupumua na changamoto za lishe. Endapo huduma sahihi haitapatikana kwa wakati, hatari ya vifo huongezeka,” alisema Dk. Kyando.

Kutokana na uwepo wa hali hiyo, alisema hospitali inahitaji kuongezewa mashine za Neonatal Radiant Warmer na Phototherapy ili kuongeza uwezo wa kuhudumia watoto wachanga, kupunguza rufaa zisizo za lazima kwenda hospitali za mikoa jirani na kuboresha ubora wa huduma kwa ujumla.

kwa upande wake,Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani na Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk. Kessy Ngalawa, alisema mashine za Phototherapy na Radiant Warmer ni muhimu katika kudhibiti joto la mwili wa mtoto mchanga na kutibu homa ya manjano (jaundice), hali inayoweza kuhatarisha maisha endapo haitashughulikiwa kwa wakati.

Dk Ngawala alitaja  kauli mbiu ya hospitali ya “Huduma Bora ni Kipaumbele Chetu.”,jambo linalowasukuma kuhakikisha wanawahudumia wananchi licha ya changamoto za kifedha na miundombinu, hospitali inaendelea kuboresha huduma kwa kuhakikisha watumishi wa afya wanafanya kazi kwa ufanisi na kuzingatia viwango vya kitaaluma.

Jan 26, 2026

TAKUKURU YAOKOA SH. BIL. 60.2


 TAKUKURU YAOKOA SH BILIONI 60.2, YAIMARISHA MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA

Na Thadei Hafigwa

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imefanikiwa kuokoa zaidi ya Shilingi bilioni 60.2 katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2025, kupitia operesheni mbalimbali za uchunguzi wa vitendo vya rushwa nchini.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila, wakati akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wa TAKUKURU uliofanyika mkoani Morogoro, Januari 26, 2026.

Bw. Chalamila alisema fedha hizo zilirejeshwa Serikalini na nyingine kutumika katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kama ilivyokusudiwa, hatua iliyochangia kuimarisha ustawi wa wananchi na kulinda rasilimali za umma.


Alifafanua kuwa, katika kipindi hicho hicho, TAKUKURU ilifuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo 619 yenye thamani ya Shilingi bilioni 553.45 na kuokoa Shilingi milioni 173.5 zilizokuwa hatarini kupotea kutokana na vitendo vya rushwa.

“Mafanikio haya yametokana na ushirikiano wa wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi pamoja na uwezeshaji mkubwa unaotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema Bw. Chalamila.

Aliongeza kuwa TAKUKURU imeendelea kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa kwa kuzingatia Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Sura ya 329, inayotaka taasisi hiyo kushirikiana na wadau mbalimbali ili kutokomeza rushwa na kukuza utawala bora nchini.

Katika hatua ya kuimarisha uelewa wa jamii, TAKUKURU imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya rushwa kupitia mikutano ya hadhara, maonesho, vipindi vya redio na televisheni, semina, warsha pamoja na machapisho mbalimbali kuanzia vijijini hadi mijini.


Bw. Chalamila pia alisema TAKUKURU, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), imefanikiwa kuingiza maudhui ya mapambano dhidi ya rushwa katika mitaala ya shule na vyuo, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kujenga kizazi chenye misingi ya uadilifu na uwajibikaji.

Kuhusu utekelezaji wa haki, alisema katika kesi 489 zilizoendeshwa mahakamani, Jamhuri ilishinda kwa asilimia 68.8 ya kesi zilizotolewa uamuzi, huku akieleza matumaini kuwa kiwango hicho kitaongezeka ifikapo Juni 2026.

Aidha, TAKUKURU iliendelea kujiimarisha kimataifa kupitia ushiriki wake katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ambapo Tanzania iliongoza Kamati Ndogo ya Kupambana na Rushwa (SACC) na kushiriki katika ufuatiliaji wa chaguzi katika baadhi ya nchi wanachama.


Katika hotuba yake, Bw. Chalamila pia alieleza kuwa TAKUKURU inaendelea kutekeleza Programu ya TAKUKURU Rafiki inayolenga kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika utoaji wa huduma za umma, ili kuzuia mianya ya rushwa kabla haijatokea.

Kwa upande wa uwajibikaji wa kijamii, alisema taasisi hiyo imeendelea kutoa msaada wa vifaa tiba kwa hospitali za rufaa, ikiwemo mashine za kuwahudumia watoto njiti, hatua inayolenga kuimarisha afya ya jamii na kudumisha uhusiano mwema kati ya TAKUKURU na wananchi.

Alisisitiza kuwa mapambano dhidi ya rushwa ni jukumu la kila mmoja, akiwataka wananchi, vyombo vya habari, sekta binafsi na taasisi za umma kuendelea kushirikiana na TAKUKURU kwa kuzingatia kaulimbiu ya taasisi hiyo isemayo: “Kuzuia Rushwa ni Jukumu Lako na Langu; Tutimize Wajibu Wetu.”

Serikali ya Awamu ya Sita inachukua Rushwa-Waziri Mkuu

WAZIRI MKUU DKT.MWiGULU NCHEMBA

Serikali ya Awamu ya Sita Inachukia Rushwa-Waziri Mkuu

Na Mwandishi wetu,Morogoro

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejizatiti kikamilifu katika mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa fedha za umma kwa kusisitiza misingi ya uadilifu, uwajibikaji na uwazi katika utendaji wa kazi serikalini.

Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2024/2025 wa Viongozi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) uliofanyika mkoani Morogoro, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Askofu wa Kanisa katoliki,jimbo la Morogoro,Mhashamu Lazarus Nsimbe(SDS) akisalimiana na mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU,Crispin Chalamila,muda mfupi baada ya mkutano mkuu wa mwaka 2024/2025 kufunguliwa mjini Morogoro.

Alisema Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa TAKUKURU katika kudhibiti vitendo vya rushwa nchini, akibainisha kuwa bila uwepo wa taasisi hiyo, rushwa ingeathiri kwa kiwango kikubwa utoaji wa huduma muhimu za kijamii kwa wananchi.

“Watanzania tunawapenda TAKUKURU. Ni taasisi muhimu katika kulinda rasilimali za umma na kuhakikisha haki inatendeka,” alisema Dkt. Nchemba, huku akiwataka wananchi kushirikiana na taasisi hiyo kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kwa wakati
Aidha, aliwataka viongozi na watumishi wa TAKUKURU kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na ujasiri, akisisitiza kuwa kazi wanayoifanya ni kwa maslahi mapana ya taifa.

Baadhi ya washiriki wa mkutano mkuu wa viongozi wa TAKUKURU nchini wakifuatilia kwa karibu hotuba ya Mgeni Rasmi,Waziri Mkuu Dkt.Mwibulu Lameck Mchumba(hayupo pichani)

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliipongeza TAKUKURU kwa mafanikio makubwa ya kuokoa shilingi bilioni 60.2 za fedha za umma katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025. Alisema kati ya kesi 489 zilizofikishwa mahakamani, asilimia 68.8 Jamhuri imeshinda, jambo linaloonesha ufanisi wa taasisi hiyo katika mapambano dhidi ya rushwa.

Alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na uwezeshaji wa Serikali pamoja na msukumo wa Rais Samia Suluhu Hassan katika kusimamia misingi ya uwajibikaji na utawala bora.

Dkt. Nchemba alionya kuwa rushwa inadhalilisha utu wa mwananchi, inadhoofisha utoaji wa huduma za kijamii na kuinyima nchi rasilimali muhimu kwa maendeleo. Kutokana na hali hiyo, aliwahimiza wadau wa elimu kuwajengea watoto mashuleni maadili ya kuchukia rushwa tangu wakiwa wadogo.

Pia aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya rushwa na kutoa maamuzi kwa wakati, hali inayochangia kuongeza imani ya wananchi katika mfumo wa haki.

Akizungumzia mianya ya rushwa, Waziri Mkuu alisema upotevu mkubwa wa fedha za umma unatokea katika maeneo ya makusanyo na matumizi ya fedha, hasa pale ambapo kunakuwa na mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watu na fedha. Alisisitiza umuhimu wa kuziba mianya hiyo kwa kuboresha mifumo na kurekebisha sheria.

Aliitaka pia Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kushirikiana kwa karibu na TAKUKURU ili kudhibiti rushwa na kuimarisha uwajibikaji miongoni mwa viongozi wa umma.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, baadhi ya miradi ya maendeleo husuasua kutokana na fedha kugawanywa kabla ya utekelezaji, akibainisha kuwa suluhisho ni kuimarisha mifumo ya kisheria na kiutawala ili kuboresha utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya, maji na miundombinu ya barabara.

Mkutano huo umehudhuriwa na washiriki 282 kutoka Tanzania Bara pamoja na viongozi saba kutoka Ofisi ya TAKUKURU Zanzibar, hatua inayolenga kuimarisha mshikamano na ufanisi wa mapambano dhidi ya rushwa nchini.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU,  Crispin Chalamila, alisema mkutano huo unawakutanisha jumla ya viongozi 234 wa TAKUKURU kutoka Makao Makuu, mikoa, wilaya na vituo maalum, pamoja na viongozi saba kutoka Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Zanzibar (ZAECA).

Chalamila alitumia fursa hiyo kumtambulisha mgeni rasmi na viongozi mbalimbali wa TAKUKURU, akibainisha kuwa taasisi hiyo pia inashirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya rushwa.

Naye Waziri wa nchi,ofisi ya Rais,utumishi na utawala bora,Ridhiwan Kikwete alisema ya kuwa TAKUKURU imekuwa ikiwezeshwa mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba kasi ya utendaji wao wa kazi inakuwa na tija kwa nchi kwa kila wilaya kupatiwa gari moja na magari mawili kwa kila mkoa. 
Kikwete alisema kuwa hatua ya serikali kuweka nguvu katika kuimarisha utendaji wa kazi takukuru ni wazi kilichopo ni kusubiri matokeo chanja kutokana na uwekezaji wa miundombinu ya majengo,na kuongeza rasilimali watu uweze kuleta matokeo chanja na tija kwa taifa.

Dec 3, 2025

TAWA WAPEWA MKAKATI USALAMA WA BINADAMU NA WANYAMAPORI

 WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII,DKT.ASHATU KIJAJI(MB) 

MAKALA MAALUM

 ZIARA YA   KIMKAKATI WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII MKOA WA MOROGORO

Na Thadei Hafigwa

 ILIKUWA ni ziara ya kimkakati  aliyoifanya  WAZIRI wa maliasili na Utalii,Dkt.Ashatu Kijaji(MB) ambapo ilitoa mwelekeo na maelekezo kwa mamlaka ya wasimamizi wa wanyamapori Tanzania(TAWA) kwa kutaja vipaumbele kwa kuzingatia  maagizo ya Rais wa Jamhuri Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan yaweze kutekelezwa kwa vitendo kwa masilahi ya nchi.

Waziri Kijaji amebainisha hayo mijini Novemba 24 Morogoro akiwa katika ziara yake ya kwanza toka ateuliwe kushika wadhifa huo katika kipindi cha pili cha awamu ya sita ya Rais Samia na kuongea na menejimenti ya TAWA,sanjari na kushiriki kwenye hafla ya kuzindua vitendea kazi kwa menejimenti na watumishi wa taasisi ya TAWA ambavyo ni magari 4,Pilipiki 33 na ndegenyuki ikiwa ni mkakati wa kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi wao.

Dkt.Kijaji alirejea hotuba aliyoitoa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan wakati akizindua bunge la 13 aliyoelekeza wizara ya maliasili na utalii na tasisi zake kuhakikisha wanaendelea kuimarisha ulinzi wa maeneo ya hifadhi na udhibiti wa wanyamapori na waharibifu dhidi ya mali na maisha ya wananchi.

Alisema kuwa,tayari serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan imeshaelekeza na kutoa nafasi ya kuajili watumishi na askari wa wanyamapori ili kwenda kuwahudumia wananchi na kupunguza kero dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yao.

”tunatakiwa tuendelee na ujenzi wa vituo vya ulinzi,tunatakiwa kuwa na mbinu za kisasa zaidi,na vifaa pia vya kisasa ikiwemo ndegenyuki,ambavyo tumezindua,tumizindua  magari,tumezindua pikipiki kwa hiyo hatuna visingizio tena kushindwa kuwahumia twendeni tukawadumie wananchi wetu”alisema.

“hivyo tunatakiwa kwenda kufanyakazi ya huduma kwa wananchi wetu  kwa kujali utu wao”

Waziri aliitaka menejimenti ya TAWA kujipanga katika kuhakikisha ya kuwa wanakwenda kutekeleza maelekezo hayo kwa weledi ili watanzania kuendelea kunufaika na rasilimali zao walizojaliwa na Mwenyezi mungu.

Aliwakumbusha kutambua kuwa msingi wa uwepo wa taasisi ya tawa ni  ulinzi wa wanyamapori bila ya kuwepo kwa jambo hilo hakutakuwemo kwa taasisi hiyo,hivyo wanapaswa  kuongeza ufanisi wa doria,itelejensia na matumizi ya teknolojia,ndegenyuki,kisukuma mawimbi,na vifaa rafiki vya ulinzi ili kulinda rasilimali muhimu zilizopo hapa nchini.

Aidha,mkakati mwingine alitaja ni kuzuia kwa kiwango cha juu vitendo vya ujangili ,uharibifu wa mazingira na biashara haramu za nyara ya serikali.

Waziri wa Maliasili na Utalii,Dkt Ashatu Kijaji(katikati) akikata utepe katika hafla ya uzinduzi wa vitendea kazi kwa maafisa wa wanyamapori mjini Morogoro alipofanya ziara ya kikazi,wengine walishiriki kushika utepe kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ta wanyamapori Tanzania(TAWA),Meja Jenerali Mstaafu,Hamis Semfuko,Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii,Hamad Chande,kutoka kushoto kwa Mhe.Waziri Kijaji ni Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA),Mlange Kabange

Pia,alihimiza kuendelea ushirikiano na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha maeneo yote chini ya tawa yanabaki salama na hakina anayeyachezea.

Suala lingine aliloliwekea kipaumbele ni kuhusisha mifumo ya taarifa,uchaguzi na tathmini ya matukio ili maamuzi ya kiutendaji yawe haraka,sahihi na yakiufanisi zaidi.

Alisisitiza na kuagiza kwamba hawatavumilia upotevu wa rasilimali za taifa,kwa kuwa Tawa wamewezeshwa kwa rasilimali  zote na utayari wa serikali ya awamu ya sita ni mkubwa katika kuhakikisha inaendelea kuweka mazingira  wezeshi ili kurahisha kutendaji kazi kwa urahisi zaidi.

Aidha,Waziri huyo wa maliasilia na utalii aliwataka tawa kuimarisha mapato na uendelevu wa taasisi kwa kujenga uwezo wa kifedha utakawezesha kulinda na kuendeleza maeneo yote walioaminiwa na kukabidhiwa na watanzania.

Alitoa maelekezo ya kuendelea kumaisha ukusanyaji wa mapato,kuhakikisha hakuna uvujaji na kuongeza ufanisi wa mifumo ya kifedha,ni muhimu sana mifumo ikasomana.

Aliweka mkazo kwa menejimenti ya tawa wa matumizi ya teknolojia katika ukusanyaji wa mapato ndani ya taasisi na kamwe kutoruhusu ukusanyaji wa fedha zikiwa mbichi,na kutumika zikiwa mbichi ili kuleta ufanisi na kurahisa kufanya tathimini kilichokusanya na kutumika katika mwaka uliopita.

Kadhalika aliwataka kuboresha fursa za uwekezaji rafiki hususan zenye tija katika mazingira yanayowazunguka katika maeneo ya utalii wa ekolojia kwa kuweka kambi za kitalii,utalii wa picha kwa kuonesha uwezo katika utendaji kazi.

Alihimiza menejimenti ya tawa kuongeza juhudi ya utangazaji wa vivutio vya utalii vilivyopo katika maeneo yote ya Tawa ili kuongeza idadi ya watalii wa ndani na nje,kwa ubunifu mbinu gani zitakazotumika katika kufanikisha jukumu hilo na kuibua vivutio vingine ili kufikia idadi ya watalii mil.8 kama ilivyoelekezwa katika ilani ya ccm 2025-2030.

“ni wazi tukafahamu bila ya  mapato hakuna maendeleo uendelevu wa taasisi yetu wala ya taifa letu,moja ya taasisi zinazotakiwa kuongeza mapato ni pamoja na taasisi yetu(tawa)”alisema

Alisema kila mmoja  alimsikia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia kwamba kipindi hiki ni cha kutumia rasilimali zilizopo hapa nchini,kutumia mapato ya ndani ili kuweza kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo nchini.

Suala lingine alilosisitiza ni utoaji wa huduma kwa wananchi ni lazima ziweze kuzingatia utu,kwamba dhamira ya serikali ni kuwatumia watu kwa utu,heshima na haki,hivyo migongano katika ya watu na wanyamapori ishughulikiwe kwa haraka kwa kutumia uadilifu,weledi na vifaa na miundombinu ilivyopo katika kuwahudumia wananchi kwenye maeneo yao.

Alikemea tabia walionayo baadhi ya watumishi wa tawa ya kuwataka wananchi kuchangia gharama za mafuta.

“ipo tabia ya kuwaambia wananchi,kama unataka nije changia mafuta,jambo hilo halipo na katibu mkuu hili naomba ulisimamie ,mwananchi hatakiwi kuchangia mafuta ili askari wetu akifikie mwananchi,ipo tabia kwa baadhi ya maeneo.”alisema

Awali,Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA),Mlange Kabange,asema wapo tayari kuteleza maagizo yote yanayotolewa na serikali katika kuhakikisha malengo ya kuwahudumia wananchi yanafikiwa kikamilifu katika uhifadhi wa wanyamapori.

Kabange anasema kuwa tawa inajukumu la kusimamia mapori ya nje ya Tanapa na  Ngorongoro,wanasimamia mapori ya akiba 28,na mapori tengevu 23,yote kwa pamoja yana ukubwa wa kilometa za mraba 133,276.36,eneo hilo ni kubwa zinazidi ukubwa wa baadhi ya nchi.

Alisema kuwa tawa wanatambua kuwa wana jukumu la kuhakikisha rasilimali za wanyamapori  zinalindwa na kwamba wafanikio wanayopata yanatokana na serikali ya awali ya sita imekuwa ikiwapatia fedha za kuteleza bajeti zao kwa asilimia 100 kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Alisema mbali ya fedha za bajeti,Rais Samia aliwapatia fedha za kuboresha miundombinu za utalii,katika kipindi cha oviko sekta nyingi zilitetereka, lakini tawa walipewa fedha bil 12.9 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya utalii.

Sanjari na hayo,alisema kuwa maafisa na watumishi wa tawa waliongezewa mshahara na watumishi 3000 wenye sifa walipandishwa vyeo jambo ambalo ni rekodi ambayo haijawahi kutokea toka kuasisiwa kwa tawa.

Aliishukuru serikali kupitia Rais Samia kuwa sekta ya utalii imekuwa kutokana na filamu ya royal tour na kupelekea mwaka jana (2024) walipata kampuni ya uwekezaji kutoka china katika sekta ya utalii,jambo ambalo siku za nyuma halijawahi kutokea.

Aidha,alishukuru wizara ya maliasili na utalii kwa kuandaa miongozo,sera na kanuni zinazowarahishia taasisi kutekeleza majukumu yake sekta ya utalii wa uwindaji na utalii wa picha.

Naye,Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ta wanyamapori Tanzania(TAWA),Meja Jenerali Mstaafu,Hamis Semfuko alimpongeza Rais Samia kwa kupata ridhaa ya kuongeza taifa la Tanzania kwa kipindi cha pili cha awali ya sita,ambapo inatokana na imani waliokuwa nayo wananchi kwake na uchapakazi wake katika sekta mbalimbali.

Meja Jenerali Mstaafu Semfuko pia alionesha shukrani zake kwa serikali kwa kuweka mazingira wezeshi katika utekelezaji wa majukumu ya tawa katika ulinzi na uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake.

 Kwa upande wake Katibu wa Wizara ya Maliasili na Utalii,Dkt.Hassan Abbas alisema ziara waliifanya ni kutembelea jeshi la uhifadhi kujua kazi zinafanyika,mafanikio na changamoto zilizopo kwa wananchi wanaishi karibu na maeneo ya hifadhi na namna ya kukabiliana nazo.

Dkt. Abbas ametaja Tanzania inaongoza kuwa na simba wengi duniani wapatao 17,000,jumla ya chui 24,000 ambapo Tanzania inaongoza Afrika na duniani,huku idadi ya ni nyati 200,025,na tembo 60,000.

Sep 20, 2025

MGOMBEA UBUNGE ATOA MATUMAINI MAPYA KWA WANANCHI MOROGORO KUSINI

Mgombea ubunge Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume

Na Thadei Hafigwa

WANANCHI wa Jimbo la Morogoro Kusini wameanisha kero na kuziwasilisha kwa Mgombea ubunge kwa tiketi cha chama cha Mapinduzi,Zuberi Mfaume ili zipatiwe ufumbuzi ikiwemo changamoto za miundombinu ya barabara,maji, uchungaji holela wa mifugo ilinayoharibu mazao ya wakulima shambani husuan kipindi cha kilimo.

Wakazi wa Kata ya Selembala,Kisaki,Mvuha,Mngazi na Bwakila chini Morogoro vijijini wamebainisha hayo kwa nyakati tofauti kwenye mikutano kampeni inayoendelea jimboni humo ambapo wameonesha imani walionayo Mgombea ubunge wa ccm jimbo la Morogoro kusinijambo lililowalazimu wagombea wengine kutoka vyama vingine vya kisiasa walionesha nia ya kuwania nafasi ya ubunge wa jimbo hilo  kutorudisha fomu walizochukua tume huru ya taifa ya uchaguzi.

Zuberi Mfaume ni Mgombea pekee ubunge Jimbo la Morogoro kusini kwa tiketi ya CCM ambaye Oktoba 29, 2025 siku ya Kupiga kura atapigia kura ya Ndiyo au Hapana kwenye kinyang’anyiro hicho.

Wagombea nafasi ya udiwani na Mgombea Ubunge,Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume wakiwa katika picha ya pamoja baadhi ya viongozi wa ccm wilaya ya Morogoro vijijini,mara baada ya kumaliza harakati za kunadi Ilani ya CCM 

Mfaume akiwa katika mikutano yake ya kampeni katika kata ya Selembala,Mvuha,Kisaki,Mngazi na Bwakila Juu, amejitwika mzigo wa changamoto zinazowakabili wananchi wa  maeneo hayo ambazo ni miundombinu ya barabara,uchungaji holela wa mifugo ambayo inaharibu mazao ya wakulima,stakabadhi ghalani pamoja na pungufu wa maji katika maeneo ya vijijini ambayo kwa mujibu wa sera ya maji,inayoelekeza wakazi wa vijijini wanapaswa kufikiwa huduma ya usambazaji wa maji kwa asilimia 85.

amewahakikishia wananchi wa maeneo hayo kuwa changamoto zinazowakabili zitashughulikiwa mara  baada ya kuchaguliwa kuhudumu nafasi ya ubunge kwa kuwa tayari ashaandaa mkakati maalum wa kuzipatia ufumbuzi changamoto zilinazowakabili  wananchi,.

“kipaumbele changu cha kwanza nitaimarisha ofisi ya mbunge kwa kuweka  dawati la msaada wa sheria ili kuwasaidia wananchi kukabiliana na changamoto za kisheria”alisema.

Mgombea huyo mbali na taaluma nyingine alizonazo pia ni mwanasheria, alinukuu ahadi iliyoanishwa kwenye Ilani ya CCM 2025-2030 iliyoelezea utatuaji wa changamoto ya miundombinu ya barabara kutoka ubenazomozi hadi Mvuha.

“ahadi namba 265 katika Kitabu cha Ilani ya chama cha Mapinduzi unasomeka Mradi wa upembuzi yakinifu katika barabara ya Ubenazomozi, Ngerengere, kuelekea kituo cha SGR,Tununguo,Selembala,Mvuha inaungana na Bigwa Kisaki kuelekea bwawa la Mwalimu Nyerere itajengwa katika kiwango cha lami”.

Harakati za kampeni zinapopamba moto viongozi wa ccm wakipongezana na Mgombea ubunge wa Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume

Rajabu Changa ni wakili msomi wa Mahakama kuu Tanzania, katika maoni yake ameshauri namna ya kutatua migogoro mingi iliyopo katika maeneo ya vijijini inatokana na kukosekana kwa uwelewa katika masuala ya sheria hususan sheria ya Ardhi na.4 ya mwaka 1999 na sheria ya KIjiji na.5 ya mwaka 1999.

“pamoja kutambua sheria hiyo ya ardhi na vijiji katika kutatua changamoto za migogoro ya ardhi inapaswa wanakijiji kuunda sheria ndogondogo na kutambua Sheria ya serikali za Mitaa,Mamlaka ya Wilaya,Sura 287 toleo la mwaka 2023,kwamba kifungu  cha 170 kinaeleza Mamlaka ya serikali ya Kijiji kutunga sheria zake,village by laws”alisema.

Alibainisha ya kuwa,Kata ya Selembala imeingizwa katika barabara kuu inayotoka Ubenazomozi mpaka  Mvuha ambayo tayari imeingizwa katika upembuzi yakinifu ili ijengwe kwa kiwango cha rami,kwamba imetafsiriwa kama barabara kuu kuelekea katika bwawa kubwa la kufufua umeme,Bwawa la Nyerere.

Pia, Mgombea Ubunge Jimbo la Morogoro Kusini ameahidi kushughulikia changamoto ya miundombinu ya barabara kutoka eneo la getini hadi Kijiji cha Kiganila kilichopo kata Selembala kwa kutumia mfuko wa jimbo.

“ninataka kuwaahidi kwamba serikali ya Chama Cha Mapinduzi ilitenga fedha maalum ya mfuko wa jimbo,moja ya kazi zake ni kutatua changamoto kama hizi,nitakuja kuwashukuru,tutakaa pamoja na tutaona namna gani tutapitisha greda walau barabara yetu iweze kupitika”alisema.

Kikosi kazi cha Chama cha Mapinduzi wakiwa na Mgombea ubunge wa Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume wapili kutoka kushoto aliyevaa shati la Kijani mwenye miwani

Aidha,alianisha changamoto nyingine ni changamoto ya vijiji viwili Bwilachini na Kibulumo vilipitiwa na mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere toka mwaka 2019 wananchi wa vijiji hivyo hawana uongozi baada ya kupatiwa eneo lingine la kuishi, la mjipya.

Mzee Zuberi Mwenegoha diwani mstaafu wa Kata ya Selembala anasema kwa sasa wananchi wanasubiri maelekezo ya uongozi wa CCM Mkoa wa Morogoro ambao wameahidi kulishughulikia suala hilo.

“kwa sasa tunasubiri uongozi wa chama cha mapinduzi Mkoa wa Morogoro ambao wameahidi kuja kututembelea na kusikiliza kero zetu ili zipatiwe ufumbuzi kwa kuwa ndicho chama chenye dola”alisema Mzee Mwenegoha.

Katika mikutano yake amekuwa alitoa elimu ya sheria umuhimu wa kuishi bila ya kubaguana kati ya wakulima na wafugaji akinukuu katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.ibara ya 13(1).

“Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki,bila ya ubaguzi wowote,kulindwa na kupata haki awa mbele ya sheria.”

Hoja hiyo imekuja baada ya wananchi kuelezea kero walionayo ya mifugo kuingia kwenye mashamba ya wakulima na kuharibu mazao. “Mkulima hana haki ya kuugua mifugo ya wafugaji,wala mfugaji hana haki ya kuingiza mifugo yake kwenye mashamba ya wakulima na kuharibu mazao.”alisema.

Aliwaahidi wananchi kumwamini kero zinazowatatiza zitawekewa utaratibu maalum wa kuzishughulikia sanjaria na kuzingatia sheria za nchi bila ya kumuonea mtu yeyote.

Temotheo Tapo kutoka jamii ya wafugaji mkazi wa  Kijiji cha Mgogoni,Kata ya Selembala amesema baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo kwenye mashamba ya watu na kuharibu mazao si jambo jema,hata hivyo aliomba serikali kuhakikisha wanawawekea mazingira mazuri ya kujengea malambo yakunyweshea mifugo.

“Mifugo yetu inakosa maji,serikali imetukataza kutumia maji ya mito kunyweshea mifugo yetu.mifugo yetu pia inakabiliwa na magonjwa ya mapafu,midomo na miguu kuvimba tunahitaji majosho”alisema Tapo.

Katika ziara ya Kampeni Zuberi alimbatana na viongozi mbalimbali wa chama,Katibu wa Vijana wa Wilaya ya Morogoro vijijini,Mussa Idowa,wajumbe  wa Kamati ya Siasa Wilaya ya Morogoro vijijini, Donny Mbena,Zamoyoni Zuberi, Scolastika Salum,Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Morogoro, na Hamza Yahya mjumbe wa halmashauri kuu CCM  Mkoa wa Morogoro.

 Kwa nyakati tofauti walinadi wagombea kwenye mikutano ya kampeni ili kuhakikisha wananchi wanajitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura na wanachagua wagombea wanaotokana na chama cha mapinduzi,Samia Suluhu Hassan katika nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Zuberi Mfaume nafasi ya ubunge pamoja na madiwani wanaogombea katika kata 17 zilizopo kwenye Jimbo la Morogoro kusini.

Kwa upande wake Mjumbe wa halmashauri kuu ccm Mkoa wa Morogoro,Hamza Yahya aliwahimiza wanachama na wapenzi wa chama hicho kuhakikisha wanawahamasisha wananchi wengine wenye sifa ya kupiga kura wanajitokeza na kukipigia kura chama cha mapinduzi ili falsafa ya mafiga matatu iweze kutekelezeka kwa vitendo,kwa kuzingatia mnyororo wa uwajibikaji wa pamoja.

Jimbo la Morogoro kusini lina jumla ya kata 17 ambazo ni Mtombozi,Selembala,Bungu,Mvuha,Kisemo,Kasanga,Konde,Lundi,Kibuko,Kolero,Tawa,Kibogwa,Bwakira chini,Kisaki,Mngazi, Bwakila juu na Singisa.

Aug 15, 2025

WANAHABARI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA SHERIA

 WANAHABARI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA SHERIA

Mwezeshaji wa mafunzo,Peter Kimath akiwasilisha mada ya usalama mitandaoni kwa wanachama wa MoroPC
Na Mwandishi wetu

WAANDISHI wahabari wametakiwa kufanya kazi kwa kuzingatia sheria ili kuepuka kuingia kwenye migogoro wakati wa kuripoti habari kuelekea katika kipindi cha uchaguzi mkuu Oktoba 2025.

Peter Kimath,Elizabeth Tanzania na Peter Laurence ni wakufunzi waliojengewa uwezo na UTPC kwa kushirikiana na IMS kwa lengo la kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari sanjari na usalama mtandaoni na masuala ya saikolojia ya maisha kwa waandishi wa habari.

Peter Kimath amesema msingi bora wa mwandishi kufanya kazi zake vizuri bila kuingia kwenye changamoto ni kufuata sheria zinazomuongoza,kufuata sheria za nchi na kuangalia sera za chombo anachofanyia kazi kwa lengo la kulisha walaji wake kile wanachotegemea

“tunapaswa kuelewa sheria na kanuni zinazohusu uchaguzi na vyombo vya habari, kama Sheria ya Huduma za Habari (2016), Sheria ya Makosa ya Mtandao (2015) na Kanuni za Tume ya Uchaguzi.”anasema Kimath.

Halfan Diyu ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo akichangia mada

Mwandishi Nguli,Halfan Diyu anasema mafunzo haya yamekuja wakati muafaka kwani yamewakumbusha vitu vingi muhimu vya kuzingatia wakati wa kuripori habari za uchaguzi na nyingine katika jamii.

“tunaishukuru UTPC na IMS  kwa kuona umuhimu wa mafunzo haya kwetu,naamini tutayatumia vizuri katika kuripoti habari,na kufuata maadili ya kiuandishi ili kuepuka kuingia kwenye msigano.

Hamida Shariff ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo anasema kutokana na teknolojia vitu vinabadilika kila siku katika tasnia ya habari,hivyo wanahabari wanapaswa kukumbushwa kila wakati katika masuala mbalimbali ikiwemo ulinzi wa taarifa binafsi na sheria zinawaongoza.

“nimejifunza vitu vizuri vitakavyonisaidia katika utendaji wangu wa kazi kila siku ikiwemo,namna ya kulinda vifaa vyangu vya kazi,kujilinda wakati wa kuripoti habari uchunguzi,UTPC nawaomba kuendelea kutoa mafunzo kama haya kwani bado wanahabari tunachangamoto nyingi zinahitaji kutatuliwa kwa njia ya kupewa elimu".

Aug 14, 2025

WANAHABARI MOROGORO WAPEWA MAFUNZO KUFANYAKAZI KWA WELEDI

 WANAHABARI MOROGORO WAPEWA MAFUNZO KUFANYAKAZI KWA WELEDI 

Baadhi ya washiriki na wanachama wa MoroPc wakifuatilia kwa umakini mafunzo yalioandaliwa na UTPC kwa kushirikana na IMS.

Na Mwandishi wetu

WANAHABARI wametakiwa kuhakikisha Wanafanya kazi kwa uhuru bila hofu ya kudhuriwa.Wanalindwa dhidi ya unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia au kisheria.

Peter Laurence,Elizabeth Tanzania na Peter Kimath ni wakufunzi waliojengewa uwezo na UTPC kwa kushirikiana na IMS kwa lengo la kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari sanjari na usalama mtandaoni na masuala ya saikolojia ya maisha kwa waandishi wa habari.

Laurence alisema waandishi wa habari wanapaswa kuongeza umakini wanapotumia mitandao ya kijamii wakati wanapotimiza wajibu wao,kwani kutawaweka salama na kuepuka kudukuliwa kazi zao.

Peter Kimath alisema kuwa waandishi wa habari wanapaswa kupewa mazingira salama ya kufanya kazi, hasa wakati wa kuripoti katika maeneo hatarishi (kama maandamano, migogoro ya kisiasa, au vita).

Mwezeshaji Peter Laurence aliwasilisha mada huku wanachama wa Moropc walifuatilia kwa karibu.

Kimath akiwasilisha mada kwa waandishi wa habari wa Morogoro kuhusu ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari alisema waandishi wa habari wazingatie weledi wanapotimiza wajibu wapo,pia wanapokabiliwa na changamoto na kadhia katika mazingira ya kazi,ambayo yanaviashiria hatarishi wawasiliane na viongozi wa Klabu za waandishi.

Mada ya saikolojia ya maisha katika mazingira ya waandishi wa habari iliwasilishwa na Elizabeth Tanzania ambaye aliwakumbusha waandishi wa habari kutambua jinsi athari ya Trauma (Kiwewe) na namna ya kukabiliana nayo.

Aliwaeleza waandishi wanapaswa kutambua maana ya trauma wa kuielezea kuwa ni hali ya maumivu makubwa ya kihisia au kiakili yanayosababishwa na tukio la kushtua sana, kama kubakwa, ajali mbaya, au kushuhudia vifo. Hali hii huweza kuathiri maisha ya mtu kwa muda mrefu.

Elizabeth Tanzania,Mwezeshaji akiwa makini katika kuwasilisha mada kwa waandishi na wanachamawa Morogoro.

“dalili ya trauma ni kumbukumbu mbaya zinazojirudia (flashbacks), kujitenga na watu, hofu au mshangao kupita kiasi,Kutojiamini, na kukosa usingizi”

Jul 27, 2025

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

 NAIBU KATIBU MKUU WA WIZARA YA ELIMU,SAYANSI NA TEKNOLOJIA,DK.HUSSEIN OMARY AKISISITIZA JAMBO.

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

WALIMU zaidi 5000 wa shule za sekondari hapa nchini kutoka kanda 7 wamenufaika na mafunzo ya  TEHAMA katika kipindi cha miaka mitatu, ambapo kwa mwaka huu pekee, walimu 1,870 wameshiriki mafunzo hayo yaliyofanyika katika vituo vya Tukuyu - Mbeya na Chuo cha Ualimu Morogoro kutokana na uwekezaji uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk.Samia Suluhu Hassan

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward Wawa alibanisha hayo katika mjini Morogoro katika hafla ya kufunga mafunzo ya awamu ya tatu kwa walimu kutoka mikoa ya Morogoro,Pwani,Dar es Saalam,Lindi na Mtwara.

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward akiwasilisha taarifa yake kwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia,Dk.Hussein Omary.

Wawa alisema kuwa kuwa serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeanza kutekeleza mradi wa kuboresha elimu ya sekondari kwa kuimarisha ujuzi wa walimu kupitia mafunzo ya TEHAMA  toka mwaka 2022 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kiashiria na 9 cha mradi wa matokeo makubwa kinacholenga kuwajengea walimu uwezo wa kufundisha kwa kutumia mbinu za kisasa na vifaa vya kidijitali.

Mafunzo hayo yametekelezwa kwa awamu tatu,kwa kuzingatia kanda 7 zilizopo,katika awamu ya kwanza,iliyofanyika mwaka 2022/2023,walimu 500 kutoka kanda ya kati na kanda ya kaskazini,walipatiwa mafunzo hayo.

“Awamu ya pili yalifanyika mwaka 2023/2024 ambapo walimu 2632 kutoka kanda ya Ziwa,kanda ya magharibi,kanda ya kaskazini na kanda ya kati,walipatiwa mafunzo”alisema.

Baadhi ya Walimu Washiriki wa mafunzo ya Tehama mjini Morogoro walifuatilia kwa umakini Hotuba ya Mgeni Rasmi,Naibu Katibu Mkuu,Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Dk.Hussein Omary (hayupo pichani) kwenye hafla ya kufunga mafunzo hayo yaliofanyika katika Chuo cha Ualimu,Morogoro.

Aidha,alifafanua kuwa awamu ya tatu ya mafunzo kwa walimu wa Tehama yamefanyika katika mwaka 2024/2025 kwa kuhusisha vituo viwili,kituo cha kwanza Tukuyu Mbeya yalianza Julai 14-18,2025 na kuwanufaisha walimu 941,na Morogoroo ambapo jumla ya walimu 929 wamenufaika na mafunzo hayo.

Mgeni Rasmi wa hafla hiyo ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Hussein Omary, ambapo ametoa wito kwa walimu nchini kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo ya kitaaluma kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, akisisitiza kuwa elimu jumuishi na yenye usawa ni msingi wa maendeleo endelevu ya taifa.

Dk. Hussein alisema kuwa serikali ina dhamira ya dhati ya kuwekeza kwa walimu ili kuimarisha elimu bora inayomfikia kila mtoto, bila kujali mahali alipo,wizara yake inaendelea kutekeleza sera ya elimu kwa vitendo, kwa kuweka mkazo katika mitaala, miundombinu, TEHAMA na maendeleo ya walimu ili kuhakikisha maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Sami Suluhu Hassan yanatimia.

“Mafunzo haya ni tafsiri ya maono ya Mheshimiwa Rais. Tunatekeleza kwa vitendo sera ya elimu jumuishi na bora. Lengo ni kuhakikisha kila mtoto anapata elimu sawa,bila kujali eneo analotoka,” alieleza.

Dk. Hussein alisisitiza nafasi ya walimu kama nguzo kuu ya mabadiliko katika mfumo wa elimu nchini, akisema mafanikio ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji wa kweli kwa walimu.

Baadhi ya washiriki wa hafla ya kufunga mafunzo kwa walimu wa sekondari juu ya TEHAMA,Mjini Morogoro

Aidha, alibainisha kuwa serikali imeanza kuimarisha miundombinu ya kufundishia kwa kutumia TEHAMA ili kukabiliana na changamoto za karne ya 21, huku akiwataka walimu kuwa mfano kwa jamii kwa kuonyesha weledi, maadili na ubunifu katika kazi zao.

Mafunzo hayo yamewahusisha walimu kutoka shule mbalimbali nchini yakiwa na malengo kuwajengea uwezo kwa kutumia vifaa na rasilimali za Tehama  darasani,kuongeza ubora wa utoaji wa elimu kupitia mbinu shirikishi za kidigitali,kuimarisha matokeo ya ufundishaji kwa wanafunzi kupitia teknolojia.

Jun 24, 2025

Waandishi wa Habari Wanawake Wajengewa Uwezo wa Kujilinda Mtandaoni na Kukabiliana na Ukatili wa Kijinsia

 Mkurugenzi Mtendaji Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC,Kenneth Simbaya

Waandishi wa Habari Wanawake Wajengewa Uwezo wa Kujilinda Mtandaoni na Kukabiliana na Ukatili wa Kijinsia

Na Mwandishi wetu, Morogoro

WAANDISHI wa habari wanawake kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar wanapatiwa mafunzo ya siku nne kuhusu usalama wa kidijitali na mbinu za kukabiliana na ukatili wa kijinsia mtandaoni, lengo likiwa ni kuwawezesha kujilinda na kutekeleza majukumu yao kwa usalama katika mazingira ya kidijitali yanayoendelea kubadilika kwa kasi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo mjini Morogoro, Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Kenneth Simbaya, alisisitiza umuhimu wa waandishi wa habari wanawake kufanya kazi kwa weledi ili kuhimili ushindani katika soko la habari linaloongozwa na maendeleo ya teknolojia ya habari na mawasiliano.

“Teknolojia imeleta mapinduzi makubwa katika sekta ya habari. Sasa mwandishi anaweza kuripoti kutoka mahali popote kupitia majukwaa ya kidijitali. Ni muhimu waandishi wanawake nao wawe sehemu ya mapinduzi haya kwa kumiliki na kuendesha vyombo vya habari vya mtandaoni,” alisema Simbaya.

Ameongeza kuwa, licha ya hofu za awali kuhusu matumizi ya intaneti, hivi sasa teknolojia hiyo imekuwa nyenzo muhimu ya kurahisisha upashanaji wa taarifa, huduma za kifedha, na mawasiliano kwa ujumla. UTPC itaendelea kuhakikisha kuwa klabu za waandishi nchini zinaendelea kwenda sambamba na kasi ya maendeleo hayo ya kidijitali.

Baadhi ya Washiriki wa mafunzo kwa Waandishi wa Habari Wanawake juu ya athari za ukatili wa kijinsia mitandaoni yaliondaliwa na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC)

Kwa upande wake, Lilian Lucas, Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Mjumbe wa Bodi ya UTPC, alisema kuwa mafunzo hayo yamewaleta pamoja waandishi wa habari wanawake kutoka mikoa 25 ya Tanzania, yakiwa na lengo la kuongeza uelewa kuhusu changamoto na athari za ukatili wa kijinsia mtandaoni.

“Ukatili wa kijinsia mtandaoni ni kikwazo kikubwa kwa uhuru wa kujieleza, ushiriki wa wanawake katika mchakato wa kidemokrasia, na heshima ya wanawake na wasichana katika jamii. UTPC ina jukumu la kuhakikisha kuwa waandishi wanawake wanakuwa na maarifa ya kutosha ya usalama wa kidijitali. Hili si jambo la hiari tena, bali ni hitaji la lazima,” alisema Lilian.

          Lilian Lucas, Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Mjumbe wa Bodi ya UTPC.

Alisisitiza kuwa washiriki wa mafunzo hayo wanapaswa kuwa mabalozi wa mabadiliko chanya, si tu katika maisha yao binafsi, bali pia katika namna wanavyoripoti habari zinazogusa sera, maisha ya watu, na kuleta mabadiliko katika jamii.

Victor Maleko, Afisa Programu wa Mafunzo na Machapisho kutoka UTPC, alisema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha waandishi wanawake kutambua hatari zilizopo katika mazingira ya mtandaoni na kujifunza mbinu mbadala za kujilinda.

“Usalama wa mwandishi unaanzia kwake mwenyewe. Mwandishi anaposhiriki kuripoti, hususan katika muktadha wa uchaguzi au maandamano, ni muhimu kuvaa mavazi yasiyoonesha upendeleo wa kisiasa na kuwa katika maeneo salama yanayowezesha kuondoka haraka endapo hali ya usalama itakuwa hatarishi,” alisema Maleko.

Mafunzo haya yameandaliwa na UTPC kwa ushirikiano na mashirika ya International Media Support (IMS), Jamii Forums, Nukta Africa, na TAMWA. Maleko alitoa wito kwa vyombo vya usalama na vyama vya siasa kutambua wajibu wao katika kuwalinda waandishi wa habari, hasa wanawake ambao mara nyingi hukumbana na madhila zaidi wanapotekeleza majukumu yao ya kitaaluma.

Kwa mujibu wa takwimu za UTPC, mwaka 2024 kulirekodiwa matukio 20 ya ukatili dhidi ya waandishi wa habari, yakiwahusisha waandishi 28. Mwaka 2023, matukio yalipungua hadi 18, huku mwaka 2021/2022 yakifikia 23. Upungufu huo unahusishwa na ongezeko la mafunzo kuhusu ulinzi na usalama kwa wanahabari.

Hata hivyo, taarifa kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) zinaonesha kuwa mwaka 2023 pekee, asilimia 77 ya waandishi wa habari wanawake waliripoti kukumbwa na aina fulani ya ukatili, hususan kupitia mitandao ya kijamii.

Jun 22, 2025

Serikali Yapongeza CAMFED Tanzania kwa Uwekezaji Madhubuti katika Maendeleo ya Wasichana

 Bi. Rhoda Sheba, Afisa Elimu wa Watu Wazima, Elimu Nje ya Mfumo Rasmi na Elimu Maalum,Mkoa wa Morogoro.

Serikali Yapongeza CAMFED Tanzania kwa Uwekezaji Madhubuti katika Maendeleo ya Wasichana

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

Serikali kupitia Ofisi ya Elimu Mkoa wa Morogoro imepongeza Shirika la CAMFED Tanzania kwa mchango mkubwa katika kuwawezesha wasichana kielimu, kijamii na kiuchumi—juhudi zinazotajwa kuwa nguzo muhimu katika ustawi wa taifa.

Pongezi hizo zilitolewa kupitia hotuba ya Afisa Elimu wa Mkoa wa Morogoro, iliyosomwa kwa niaba yake na Bi. Rhoda Sheba, Afisa Elimu wa Watu Wazima, Elimu Nje ya Mfumo Rasmi na Elimu Maalum,Mkoa wa Morogoro wakati wa ufunguzi wa Kongamano la  mafunzo maalum kwa wasichana waliomaliza sekondari na kufadhiliwa na CAMFED,iliyojumuisha Wilaya za Iringa,KILOLO,Chamiwino,Morogoro vijijini,Mlimba ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kujiunga na vyuo vya kati na vyuo vikuu.

“CAMFED siyo tu inatoa ufadhili wa masomo, bali inajenga mfumo wa ufuatiliaji wa maendeleo ya kielimu na maisha ya baadaye ya wanufaika wake. Huu ni mfano wa kuigwa katika kujenga kizazi imara cha wasomi na viongozi wa kesho,” alisema Bi. Sheba.

Aliongeza kuwa amewahi kushuhudia mnufaika wa CAMFED aliyekuwa likizo kutoka chuo kikuu akijitolea kuwahamasisha na kuwaelekeza wasichana walioko sekondari—ishara ya ushawishi chanya wa mpango huo katika kuendeleza mnyororo wa mafanikio.

Takwimu za mwaka 2024 zinaonesha kuwa CAMFED Tanzania imefadhili zaidi ya wasichana 154,201, na idadi hiyo imeokwenda sambamba na ngezeko la ufaulu katika mitihani yao ya kidato cha nne katika elimu ya sekondari, hatua iliyopokelewa kwa shangwe na pongezi kutoka kwa washiriki wa Kongamano hilo.

“Ni jambo la kujivunia kuona idadi kubwa ya watoto wa kike wakifanikiwa licha ya changamoto lukuki zinazowakabili. Mafanikio haya yanaonesha wazi kuwa uwekezaji kwa mtoto wa kike ni uwekezaji wenye tija kwa taifa,” aliongeza Bi. Sheba.

Washiriki wa Kongamano la Mafunzo maalum kwa Wanachuo tarajali,lilikofanyika katika shule ya Sekondari ya Kilakala,Morogoro wakifuatilia kwa umakini hotuba ya Mgeni Rasmi.

Mafunzo na Uwezeshaji wa Viongozi wa Baadaye

Mbali na ufadhili wa masomo, CAMFED Tanzania inatekeleza programu mbalimbali za kuwajengea uwezo wasichana katika uongozi, ujasiriamali, na stadi za maisha kupitia kwenye shule za sekondari.

Akizungumza katika Kongamano hilo la mafunzo, Mkuu wa Idara ya Miradi wa CAMFED Tanzania, Bi. Dominica Lyambo, alibaisha program ya kuwajengea uwezo wasichana uwezo kuelekea kujiunga na vyuo ni shule ya sekondari Kilakala (Morogoro), Ng’anza (Mwanza), na Shule ya wasichana ya Mkoa wa Pwani.

Lyambo alisema shirika hilo linafanya kazi katika nchi tano za Afrika ambazo ni Tanzania, Zambia, Zimbabwe, Ghana, na Malawi.

Mkuu wa Idara ya Miradi wa CAMFED Tanzania, Bi. Dominica Lyambo akiwasilisha taarifa yake,Mjini Morogoro katika Kongamano la wasichana ambao ni wanachuo tarajali wanaofadhiliwa na shirika lake

“Tanzania tulianza mwaka 2005 na tumesajiliwa rasmi mwaka 2006. Kwa sasa tunafanya kazi katika mikoa 10 na halmashauri 35, huku lengo la mwaka 2025 likiwa ni kufikia halmashauri 41,” alisema Bi. Lyambo.

Aliongeza kuwa CAMFED tayari imefikia halmashauri zote katika mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro, na kazi inaendelea katika mikoa mingine ili kufanikisha lengo la kufikia halmashauri zote 76 zilizopo kwenye mikoa hiyo 10.

Uwajibikaji na Ulinzi wa Mtoto

Kwa mujibu wa Bi. Lyambo, utekelezaji wa miradi ya CAMFED unazingatia misingi ya utawala bora, ikiwemo sera ya ulinzi wa mtoto, usimamizi wa rasilimali, na uwajibikaji wa kifedha. Aidha, shirika hilo linafanya kazi kwa karibu na wadau kutoka ngazi ya kijiji hadi wizara, wakiwemo maafisa ustawi wa jamii, kamati za shule, na maafisa elimu kata.

“Tunaamini mtoto wa kike akipewa mazingira salama ya kusoma, akiheshimiwa na kuthaminiwa, ana nafasi kubwa ya kufikia ndoto zake na kuondokana na umaskini,” alieleza.

Bi. Lyambo pia alibainisha kuwa mafanikio ya CAMFED yametokana na ushirikiano mzuri na wanachama wa CAMFED Association—ambao ni wanufaika waliorejea kuleta mabadiliko katika jamii zao.

Sauti za Wanufaika

Mmoja wa wanufaika wa mpango huo, Salma Salum, alieleza kuwa CAMFED imekuwa msaada mkubwa katika maisha yake kwa kumwezesha kielimu na kumwandaa kiakili na kisaikolojia kwa safari ya elimu ya juu.

“Ninaishukuru CAMFED kwa kutuwezesha siyo tu kielimu, bali pia kwa kutujengea uwezo wa kukabiliana na changamoto tunazokutana nazo tunapoingia vyuoni,” alisema.

Je, Wavulana Watasahaulika?

 CAMFED ilifafanua kuwa kwa sasa mpango huo umejikita kwa wasichana kutokana na changamoto maalum wanazokumbana nazo, lakini mjadala huo umefungua fursa ya kutafakari upanuzi wa wigo wa mnufaika katika siku zijazo.