Breaking News

Jun 1, 2026

JENGO LA TAKUKURU MOROGORO LAGHARIMU SH.1.6 BILIONI, LAIMARISHA UTOAJI WA HUDUMA KWA UMMA


MKURUGENZI MKUU WA  TAKUKURU, BW. CRISPIN FRANCIS CHALAMILA AKIONGOZA NA WADAU NA VYOMBO VYA ULINZI NA USALAMA KUKATA UTEPE KUASHIRIA UZINDUZI WA JENGO HILO

 JENGO LA  TAKUKURU MOROGORO LAGHARIMU SH.1.6 BILIONI, LAIMARISHA UTOAJI WA HUDUMA KWA UMMA

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

SERIKALI ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha misingi ya utawala bora, uwajibikaji na mapambano dhidi ya rushwa kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Hatua hiyo imejidhihirisha kwa uzinduzi wa jengo jipya la Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Morogoro lililogharimu Shilingi bilioni 1.627, mradi unaotarajiwa kuongeza ufanisi wa watumishi, kuboresha utoaji wa huduma na kusogeza karibu zaidi huduma za taasisi hiyo kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa jengo hilo uliofanyika Juni 1, 2026 mjini Morogoro, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha taasisi zinazosimamia uwajibikaji zinakuwa na mazingira bora ya kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.


             MUONEKANO WA JENGO LA OFISI YA TAKUKURU MKOA WA MOROGORO

“Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuwekeza katika kuimarisha taasisi za mapambano dhidi ya rushwa ili ziweze kutekeleza wajibu wake kwa weledi na kwa kiwango kinachokidhi matarajio ya wananchi,” alisema Chalamila.

Alieleza kuwa TAKUKURU kwa sasa ina ofisi 145 nchini, zikiwemo ofisi za mikoa 28, wilaya 111 na vituo maalumu sita, huku ofisi 70 pekee zikiwa zinamilikiwa na taasisi hiyo na nyingine zikiendelea kujengwa kulingana na upatikanaji wa fedha za Serikali.

Kwa mujibu wa Chalamila, katika mwaka wa fedha 2025/2026 taasisi hiyo inaendelea na ujenzi wa majengo 11 mapya, yakiwemo ya mkoa mmoja na wilaya 10, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuondoa changamoto ya uhaba wa majengo ya ofisi nchini.

                  MKURUGENZI MKUU WA  TAKUKURU, BW. CRISPIN FRANCIS CHALAMILA,AKISHIRIKIANA NA MKUU WA WILAYA YA MVOMERO,MAULID DOTTO AMBAYE ALIMWAKILISHA MKUU WA MKOA WA MOROGORO,ADAM MALIMA KATIKA HAFLA YA UZINDUZI WA JENGO LA OFISI YA TAKUKURU MKOA WA MROGORO.

“Bado tuna ofisi 64 ambazo hazina majengo ya kudumu. Hivyo, kukamilika kwa jengo la Morogoro ni hatua muhimu katika safari ya kuimarisha uwezo wa taasisi yetu kufikia wananchi kwa karibu zaidi,” alisema.

Taarifa ya utekelezaji wa mradi iliyosomwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Usimamizi wa Milki wa TAKUKURU, Eng. Dk. Emmanuel Kiyabo, ilieleza kuwa mradi huo ulianza Machi 6, 2025 kwa bajeti ya Shilingi 1,600,016,922.08 na kukamilika Machi 30, 2026 baada ya kuchelewa kwa takribani miezi mitatu kutokana na changamoto mbalimbali za utekelezaji.

Miongoni mwa changamoto zilizochelewesha mradi huo ni ucheleweshwaji wa vifaa vya ujenzi hususan mabati, uhaba wa baadhi ya vifaa maalumu vya ukuta wa vioo, mvua za masika pamoja na kusitishwa kwa shughuli mbalimbali kufuatia mazingira ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Mradi huo ulitekelezwa kwa mfumo wa “Design and Build” kwa ushirikiano kati ya TAKUKURU na Shirika la Magereza (PCS), ambapo wataalamu wa taasisi hizo walishirikiana katika usanifu na ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya kisasa.

MKURUGENZI MKUU WA  TAKUKURU, BW. CRISPIN FRANCIS CHALAMILA AKIMWAGILIA MTI MAJI, BAADA YA KUPANDA MOJA YA KIASHIRIA YA UZINDUZI WA JENGO LA TAKUKURU MKOA WA MOROGORO.

Jengo hilo la ghorofa moja lina eneo la sakafu lenye mita za mraba 575 na limejumuisha nyumba ya walinzi, nyumba ya mfumo wa umeme na jenereta, uzio wa kisasa wenye mageti yanayotumia mfumo wa umeme, tenki la maji la chini lenye uwezo wa kuhifadhi lita 60,000 pamoja na mnara wa matenki ya maji.

Chalamila alisema gharama za mradi ziliongezeka kwa asilimia 1.74 pekee kutoka bajeti ya awali, jambo ambalo linaonesha usimamizi mzuri wa fedha za umma katika utekelezaji wa mradi huo. Ongezeko hilo lilitokana na maboresho yaliyofanyika wakati wa utekelezaji ikiwemo kuongeza mifumo ya mageti ya umeme na kupanua eneo la paving blocks.

Mbali na uwekezaji wa miundombinu, Chalamila alisisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kusimamia matumizi ya fedha za umma na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana.

Alisema uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi ni nguzo muhimu katika kuzuia mianya ya rushwa na kujenga imani kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya rasilimali za Taifa.

Katika hatua nyingine, aliwataka watumishi wa TAKUKURU kuyatunza majengo na vifaa vinavyotolewa na Serikali ili viweze kudumu kwa muda mrefu na kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika maadili kwa vijana kupitia Klabu za Wapinga Rushwa mashuleni, akisema kuwa mapambano dhidi ya rushwa hayawezi kufanikiwa bila kujenga kizazi chenye uadilifu, uzalendo na uwajibikaji.

Aliwataka viongozi wa dini, vyama vya siasa, asasi za kiraia na wananchi kwa ujumla kushirikiana na TAKUKURU katika kuelimisha jamii kuhusu madhara ya rushwa na kuhamasisha utamaduni wa kukataa na kuripoti vitendo vya rushwa.

“Mapambano dhidi ya rushwa ni jukumu la kila Mtanzania. Ushirikiano wa wananchi ndiyo silaha kubwa katika kujenga taifa lenye uwajibikaji, haki na maendeleo endelevu,” alisema.

Uzinduzi wa jengo hilo unatajwa kuwa sehemu ya juhudi pana za Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha taasisi za umma, kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma na kuendeleza vita dhidi ya rushwa kama msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

DIRA YA TAIFA YA MAENDELEO 2050 KUTATUA CHANGAMOTO YA MAJI NCHINI-MSIGWA

 KATIBU MKUU WA WIZARA YA HABARI,UTAMADUNI NA MICHEZO,GERSON MSIGWA NA MSEMAJI MKUU WA SERIKALI

 DIRA YA TAIFA YA MAENDELEO 2050 KUTATUA CHANGAMOTO YA MAJI NCHINI-MSIGWA


Na.Nickson Mkilanya

KATIBU Mkuu Wizara ya Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amewataka Watanzania kuzingatia kwa umakini maeneo yanayoweza kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi. 

Aliyataja maeneo matatu yenye fursa ikiwemo kuajiri watu wengi, mazao yenye uwezo wa kuongezewa thamani na kuuzwa katika masoko ya nje, pamoja na sekta zenye uwezo wa kufungamanishwa na sekta nyingine ili kuongeza tija na mapato.

Alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari walipotembelea eneo la utekelezaji wa Mradi wa Kimkakati katika Bwawa la Kidunda, wilayani Morogoro, mkoani Morogoro mradi unaosimamiwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA). 

“Lazima tuongeze mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi,ili kuuza nje, mazao haya yanapaswa kuongezewa thamani.Bidhaa kama mchele, mahindi, nyama na madini lazima zizalishwe kwa ubora, zifungashwe vizuri na ziwe na sifa zinazokubalika katika masoko ya kimataifa,”alisema Msigwa.

Akizungumzia suala la kufungamanisha sekta mbalimbali, Msigwa alitolea mfano sekta za madini, kilimo, utalii na michezo, akisema ushirikiano kati ya sekta hizo unaweza kuongeza thamani ya uzalishaji na mapato ya taifa.

Aidha, alieleza kuwa Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa maeneo muhimu ya uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara nchini. Mkoa huo pia una viwanda 63 vikubwa, viwanda vya kati 1,049, viwanda vidogo 3,147 pamoja na wafanyabiashara 15,970. Alisema uwepo wa shughuli hizo za kiuchumi unahitaji mazingira ya amani na utulivu ili kuongeza uzalishaji na mafanikio.

Hata hivyo, Msigwa alisisitiza kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 hautawezekana bila kuwepo kwa amani na utulivu nchini.

“Kwa sasa nchi ni shwari, amani ipo na Watanzania wanaendelea na shughuli zao kama kawaida. Wananchi wasiwe na hofu. Changamoto zilizopo zinaendelea kutatuliwa.waendelee kupanga na kutekeleza shughuli zao za maendeleo kwa kuwa Tanzania ni nchi salama na tulivu,”alisema.

Aliongeza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii, huku amani na utulivu vikiwa nguzo muhimu za kufanikisha malengo hayo.

“Tumkatae mtu yeyote mwenye mwelekeo wa kuvuruga amani, mshikamano na umoja wetu. Hakuna nchi inayoweza kuendelea wakati watu wanatishana, wanazuiana kufanya kazi au kusababisha vurugu. Utulivu ni jukumu la kila Mtanzania,” alisisitiza.

Msigwa alisema nchi zilizoendelea zimefanikiwa kutokana na wananchi wake kufanya kazi katika mazingira ya amani na utulivu.


Alionya kuwa hali ya sintofahamu inaweza kuwakatisha tamaa wawekezaji na kusababisha wananchi kupoteza ajira.

Kuhusu upatikanaji wa maji safi, alisema Serikali kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuhakikisha wananchi wote wanapata maji safi na salama kwa asilimia 100 ifikapo mwaka 2050.

Alieleza kuwa bado kuna changamoto ya upatikanaji wa maji katika baadhi ya maeneo, hususan Dar es Salaam na Pwani, hasa kipindi cha Oktoba kila mwaka, licha ya uwepo wa vyanzo vya maji vya Ruvu Juu na Ruvu Chini.

Kutokana na changamoto hiyo, alisema Rais Samia Suluhu Hassan alielekeza kuanza kwa ujenzi wa Bwawa la Kidunda, mradi ambao hadi sasa umefikia zaidi ya asilimia 50 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu kwa gharama ya shilingi bilioni 336 za fedha za ndani.

Msigwa alisema bwawa hilo, linalojengwa na mkandarasi Sinohydro Corporation Ltd chini ya usimamizi wa DAWASA, litakuwa na uwezo wa kuzalisha lita bilioni 190 za maji yatakayotumika kwa shughuli mbalimbali, ikiwemo kusambaza maji safi na salama kwa wakazi wa Dar es Salaam, Pwani na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Morogoro.

Aliongeza kuwa maji hayo pia yatatumika kulinda ikolojia ya eneo la bwawa, kuzalisha megawati 30 za umeme zitakazoingizwa katika Gridi ya Taifa, pamoja na kusaidia uzalishaji wa miwa katika Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi na shughuli nyingine za kilimo.

Msimamizi wa Mradi wa Bwawa la Kidunda,Kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Christian Gava.

Msimamizi wa Mradi wa Bwawa la Kidunda,Kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Christian Gava alisema mradi huo umefikia asilimia 50.3 ya utekelezaji, huku kazi zote kubwa za msingi zikiwa zimekamilika kwa zaidi ya asilimia 90.

Mhandisi Gava alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Desemba 2026 na kwamba hadi sasa Serikali imeshamlipa mkandarasi zaidi ya shilingi bilioni 132, huku kukiwa hakuna madai yoyote kutoka kwa mkandarasi au mshauri wa mradi.

Aidha, alisema lita milioni 410 za maji zimetengwa kwa ajili ya shughuli za kilimo katika shamba la miwa la Mkulazi.

“Tumepokea maelekezo kutoka Serikalini na tutayafanyia kazi. Ni wajibu wetu kuhakikisha tunasimamia mradi huu kwa uadilifu kwa sababu fedha zinazotumika ni kodi za wananchi, ambao wana haki ya kujua namna zinavyotumika,”alisema.


Feb 28, 2026

CBO YAZINDULIWA MATULI KWA KUGAWA PICHA ZA VIONGOZI WA KITAIFA MASHULENI


 MATULI CBO YAZINDULIWA RASMI, YAAHIDI KUHAMASISHA MAENDELEO YA JAMII NA UHIFADHI WA MAZINGIRA


Na Mwandishi Wetu

Hatua mpya ya kuhamasisha maendeleo ya jamii imeanza kushika kasi kufuatia uzinduzi rasmi wa Matuli Community Based Organization (Matuli CBO),iliopo Kata ya Matuli, Halmashauri ya Wilaya Morogoro, taasisi ya kijamii inayolenga kutumia fursa zilizopo katika hilo, ikiwemo rasilimali za misitu, kukuza ujasiriamali kwa vijana na kuendeleza miradi ya uhifadhi wa mazingira.

Uzinduzi huo ulifanyika kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo, huku mgeni rasmi akiwakilishwa na Mwenyekiti wa CCM Kata ya Matuli, Mohaned Rashid Chenga, ambaye alipongeza uanzishwaji wa taasisi hiyo kwa kueleza kuwa ni jukwaa muhimu la kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana pamoja na kuinua kipato cha wananchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa Matuli CBO, Moses Chunga, alisema taasisi hiyo imejipanga kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutoa elimu ya uhifadhi wa mazingira, ujasiriamali, kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi pamoja na lishe bora mashuleni kwa njia ya jamii jumuishi.

Alifafanua kuwa Matuli CBO itaongozwa na dira ya kuunga mkono malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, kwa kuhakikisha jamii inatumia rasilimali zake kwa tija bila kuharibu mazingira.

“Tutahamasisha vijana kuunda vikundi vya uzalishaji mali na kuomba mizinga kwa ajili ya ufugaji nyuki katika msitu wa Matuli, kama sehemu ya kuongeza kipato na kulinda misitu yetu. Pia tuna mpango wa kuanzisha mradi wa kaboni utakaosaidia kuhifadhi mazingira na kuunga mkono juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi,” alisema Chunga.

Kwa upande wake, Deograsia Mallya Mratibu wa Miradi wa Matuli CBO aliwataka vijana kutumia fursa hiyo kwa kujiunga na vikundi vitakavyowezeshwa kupata mafunzo na mitaji midogo, akisisitiza nidhamu, uwajibikaji na mshikamano kama msingi wa mafanikio ya miradi ya kijamii.

Katika hafla hiyo, Matuli CBO pia ilinadi sera yake ya kusaidia vijana katika sekta ya sanaa, ujasiriamali na utunzaji wa mazingira. Aidha, taasisi hiyo imeahidi kumleta mdhamini wake, kampuni ya Farmer Center Limited, inayojihusisha na viuatilifu, ili kutoa elimu bure kwa wakulima na wafugaji wa Matuli kuhusu kilimo bora, matumizi sahihi ya viuatilifu na mbinu bora za ufugaji.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo walieleza matumaini yao kuwa taasisi hiyo itakuwa chachu ya mabadiliko chanya kwa vijana na wakulima, hasa katika kipindi ambacho changamoto za ajira na mabadiliko ya tabianchi zimeendelea kuathiri uzalishaji na kipato cha kaya nyingi.

Kwa uzinduzi huo, Matuli CBO imeanza safari ya kuhamasisha maendeleo ya jamii kwa vitendo, kwa lengo la kujenga jamii yenye uchumi imara, mazingira salama na kizazi chenye maarifa ya kujitegemea.

Jan 30, 2026

TAKUKURU YAGAWA VIFAA TIBA, KUOKOA MAISHA YA WATOTO NJITI

 


TAKUKURU YAGAWA VIFAA TIBA KUOKOA MAISHA YA WATOTO NJITI  MOROGORO

Na Thadei Hafigwa

KUTOKANA na changamoto zinazoikabili sekta ya afya nchini, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeazimia kufanya matendo ya huruma kwa kugawa vifaa tiba vya kisasa kwa ajili ya kusaidia watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya wakati (watoto njiti) katika hospitali zote za rufaa nchini.

Hatua hiyo ilidhihirishwa mjini Morogoro wakati wa hafla ya kukabidhi mashine mbili za Phototherapy na Neonatal Radiant Warmer kwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, hafla iliyohudhuriwa na viongozi wa hospitali hiyo pamoja na maafisa wa TAKUKURU kutoka ngazi ya mkoa na taifa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Francis Chalamila, alisema msaada huo ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuboresha huduma za afya nchini, hususan huduma za mama na mtoto.


Chalamila alisema kuwa, menejimenti ya TAKUKURU ilifanya uamuzi huo kwa misingi ya utu, busara na hekima baada ya kubaini kuwa kuna uhitaji mkubwa wa vifaa tiba katika hospitali mbalimbali nchini, hususan vifaa vya kuwahudumia watoto njiti.

“Taarifa tulizozipata kutoka vituo vya kutolea huduma za afya zinaonesha kuwepo kwa uhitaji mkubwa wa vifaa tiba, hasa mashine za kuwasaidia watoto njiti ili kunusuru maisha yao,” alisema Chalamila.

Alifafanua zaidi kwamba, ununuzi wa mashine hizo umewezeshwa na michango ya hiari kutoka kwa watumishi wa TAKUKURU, waliotoa sehemu ya mishahara yao, akibainisha kuwa taasisi hiyo haina mfuko maalumu wa uwajibikaji kwa jamii kama ilivyo kwa baadhi ya taasisi nyingine.

“Tupo katika zoezi la kugawa mashine za kuwasaidia watoto njiti katika hospitali zote za rufaa nchini. Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ni hospitali ya kumi kufikiwa, na tunaendelea kufikia mikoa mingine hivi karibuni,” alisema Chalamila.


Kwa mujibu wa Mkurugenzi mkuu wa Takukuru, hatua hiyo ni matendo ya huruma na hiyari kwa watumishi wa TAKUKURU, ambao wameguswa na uhitaji mkubwa uliopo katika jamii, sambamba na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha huduma za afya nchini.

Naye, Kaimu Mratibu wa Huduma za Tiba wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk. Azael Haward Kyando, alisema hospitali hiyo hupokea mara kwa mara idadi ya watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati, wakiwemo wenye uzito mdogo na wanaohitaji uangalizi wa karibu mara tu baada ya kuzaliwa jambo linaloashiria uwepo mkubwa wa tatizo hilo.

 “Watoto njiti hukumbwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo kushindwa kudhibiti joto la mwili, hatari ya maambukizi, matatizo ya kupumua na changamoto za lishe. Endapo huduma sahihi haitapatikana kwa wakati, hatari ya vifo huongezeka,” alisema Dk. Kyando.

Kutokana na uwepo wa hali hiyo, alisema hospitali inahitaji kuongezewa mashine za Neonatal Radiant Warmer na Phototherapy ili kuongeza uwezo wa kuhudumia watoto wachanga, kupunguza rufaa zisizo za lazima kwenda hospitali za mikoa jirani na kuboresha ubora wa huduma kwa ujumla.

kwa upande wake,Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani na Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dk. Kessy Ngalawa, alisema mashine za Phototherapy na Radiant Warmer ni muhimu katika kudhibiti joto la mwili wa mtoto mchanga na kutibu homa ya manjano (jaundice), hali inayoweza kuhatarisha maisha endapo haitashughulikiwa kwa wakati.

Dk Ngawala alitaja  kauli mbiu ya hospitali ya “Huduma Bora ni Kipaumbele Chetu.”,jambo linalowasukuma kuhakikisha wanawahudumia wananchi licha ya changamoto za kifedha na miundombinu, hospitali inaendelea kuboresha huduma kwa kuhakikisha watumishi wa afya wanafanya kazi kwa ufanisi na kuzingatia viwango vya kitaaluma.

Jan 26, 2026

TAKUKURU YAOKOA SH. BIL. 60.2


 TAKUKURU YAOKOA SH BILIONI 60.2, YAIMARISHA MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA

Na Thadei Hafigwa

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imefanikiwa kuokoa zaidi ya Shilingi bilioni 60.2 katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2025, kupitia operesheni mbalimbali za uchunguzi wa vitendo vya rushwa nchini.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila, wakati akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wa TAKUKURU uliofanyika mkoani Morogoro, Januari 26, 2026.

Bw. Chalamila alisema fedha hizo zilirejeshwa Serikalini na nyingine kutumika katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kama ilivyokusudiwa, hatua iliyochangia kuimarisha ustawi wa wananchi na kulinda rasilimali za umma.


Alifafanua kuwa, katika kipindi hicho hicho, TAKUKURU ilifuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo 619 yenye thamani ya Shilingi bilioni 553.45 na kuokoa Shilingi milioni 173.5 zilizokuwa hatarini kupotea kutokana na vitendo vya rushwa.

“Mafanikio haya yametokana na ushirikiano wa wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi pamoja na uwezeshaji mkubwa unaotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema Bw. Chalamila.

Aliongeza kuwa TAKUKURU imeendelea kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa kwa kuzingatia Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Sura ya 329, inayotaka taasisi hiyo kushirikiana na wadau mbalimbali ili kutokomeza rushwa na kukuza utawala bora nchini.

Katika hatua ya kuimarisha uelewa wa jamii, TAKUKURU imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya rushwa kupitia mikutano ya hadhara, maonesho, vipindi vya redio na televisheni, semina, warsha pamoja na machapisho mbalimbali kuanzia vijijini hadi mijini.


Bw. Chalamila pia alisema TAKUKURU, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), imefanikiwa kuingiza maudhui ya mapambano dhidi ya rushwa katika mitaala ya shule na vyuo, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kujenga kizazi chenye misingi ya uadilifu na uwajibikaji.

Kuhusu utekelezaji wa haki, alisema katika kesi 489 zilizoendeshwa mahakamani, Jamhuri ilishinda kwa asilimia 68.8 ya kesi zilizotolewa uamuzi, huku akieleza matumaini kuwa kiwango hicho kitaongezeka ifikapo Juni 2026.

Aidha, TAKUKURU iliendelea kujiimarisha kimataifa kupitia ushiriki wake katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ambapo Tanzania iliongoza Kamati Ndogo ya Kupambana na Rushwa (SACC) na kushiriki katika ufuatiliaji wa chaguzi katika baadhi ya nchi wanachama.


Katika hotuba yake, Bw. Chalamila pia alieleza kuwa TAKUKURU inaendelea kutekeleza Programu ya TAKUKURU Rafiki inayolenga kusikiliza na kutatua kero za wananchi katika utoaji wa huduma za umma, ili kuzuia mianya ya rushwa kabla haijatokea.

Kwa upande wa uwajibikaji wa kijamii, alisema taasisi hiyo imeendelea kutoa msaada wa vifaa tiba kwa hospitali za rufaa, ikiwemo mashine za kuwahudumia watoto njiti, hatua inayolenga kuimarisha afya ya jamii na kudumisha uhusiano mwema kati ya TAKUKURU na wananchi.

Alisisitiza kuwa mapambano dhidi ya rushwa ni jukumu la kila mmoja, akiwataka wananchi, vyombo vya habari, sekta binafsi na taasisi za umma kuendelea kushirikiana na TAKUKURU kwa kuzingatia kaulimbiu ya taasisi hiyo isemayo: “Kuzuia Rushwa ni Jukumu Lako na Langu; Tutimize Wajibu Wetu.”

Serikali ya Awamu ya Sita inachukua Rushwa-Waziri Mkuu

WAZIRI MKUU DKT.MWiGULU NCHEMBA

Serikali ya Awamu ya Sita Inachukia Rushwa-Waziri Mkuu

Na Mwandishi wetu,Morogoro

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejizatiti kikamilifu katika mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa fedha za umma kwa kusisitiza misingi ya uadilifu, uwajibikaji na uwazi katika utendaji wa kazi serikalini.

Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2024/2025 wa Viongozi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) uliofanyika mkoani Morogoro, akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Askofu wa Kanisa katoliki,jimbo la Morogoro,Mhashamu Lazarus Nsimbe(SDS) akisalimiana na mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU,Crispin Chalamila,muda mfupi baada ya mkutano mkuu wa mwaka 2024/2025 kufunguliwa mjini Morogoro.

Alisema Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa TAKUKURU katika kudhibiti vitendo vya rushwa nchini, akibainisha kuwa bila uwepo wa taasisi hiyo, rushwa ingeathiri kwa kiwango kikubwa utoaji wa huduma muhimu za kijamii kwa wananchi.

“Watanzania tunawapenda TAKUKURU. Ni taasisi muhimu katika kulinda rasilimali za umma na kuhakikisha haki inatendeka,” alisema Dkt. Nchemba, huku akiwataka wananchi kushirikiana na taasisi hiyo kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kwa wakati
Aidha, aliwataka viongozi na watumishi wa TAKUKURU kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na ujasiri, akisisitiza kuwa kazi wanayoifanya ni kwa maslahi mapana ya taifa.

Baadhi ya washiriki wa mkutano mkuu wa viongozi wa TAKUKURU nchini wakifuatilia kwa karibu hotuba ya Mgeni Rasmi,Waziri Mkuu Dkt.Mwibulu Lameck Mchumba(hayupo pichani)

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliipongeza TAKUKURU kwa mafanikio makubwa ya kuokoa shilingi bilioni 60.2 za fedha za umma katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025. Alisema kati ya kesi 489 zilizofikishwa mahakamani, asilimia 68.8 Jamhuri imeshinda, jambo linaloonesha ufanisi wa taasisi hiyo katika mapambano dhidi ya rushwa.

Alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na uwezeshaji wa Serikali pamoja na msukumo wa Rais Samia Suluhu Hassan katika kusimamia misingi ya uwajibikaji na utawala bora.

Dkt. Nchemba alionya kuwa rushwa inadhalilisha utu wa mwananchi, inadhoofisha utoaji wa huduma za kijamii na kuinyima nchi rasilimali muhimu kwa maendeleo. Kutokana na hali hiyo, aliwahimiza wadau wa elimu kuwajengea watoto mashuleni maadili ya kuchukia rushwa tangu wakiwa wadogo.

Pia aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kuharakisha usikilizwaji wa mashauri ya rushwa na kutoa maamuzi kwa wakati, hali inayochangia kuongeza imani ya wananchi katika mfumo wa haki.

Akizungumzia mianya ya rushwa, Waziri Mkuu alisema upotevu mkubwa wa fedha za umma unatokea katika maeneo ya makusanyo na matumizi ya fedha, hasa pale ambapo kunakuwa na mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watu na fedha. Alisisitiza umuhimu wa kuziba mianya hiyo kwa kuboresha mifumo na kurekebisha sheria.

Aliitaka pia Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kushirikiana kwa karibu na TAKUKURU ili kudhibiti rushwa na kuimarisha uwajibikaji miongoni mwa viongozi wa umma.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, baadhi ya miradi ya maendeleo husuasua kutokana na fedha kugawanywa kabla ya utekelezaji, akibainisha kuwa suluhisho ni kuimarisha mifumo ya kisheria na kiutawala ili kuboresha utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya, maji na miundombinu ya barabara.

Mkutano huo umehudhuriwa na washiriki 282 kutoka Tanzania Bara pamoja na viongozi saba kutoka Ofisi ya TAKUKURU Zanzibar, hatua inayolenga kuimarisha mshikamano na ufanisi wa mapambano dhidi ya rushwa nchini.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU,  Crispin Chalamila, alisema mkutano huo unawakutanisha jumla ya viongozi 234 wa TAKUKURU kutoka Makao Makuu, mikoa, wilaya na vituo maalum, pamoja na viongozi saba kutoka Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Zanzibar (ZAECA).

Chalamila alitumia fursa hiyo kumtambulisha mgeni rasmi na viongozi mbalimbali wa TAKUKURU, akibainisha kuwa taasisi hiyo pia inashirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya rushwa.

Naye Waziri wa nchi,ofisi ya Rais,utumishi na utawala bora,Ridhiwan Kikwete alisema ya kuwa TAKUKURU imekuwa ikiwezeshwa mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba kasi ya utendaji wao wa kazi inakuwa na tija kwa nchi kwa kila wilaya kupatiwa gari moja na magari mawili kwa kila mkoa. 
Kikwete alisema kuwa hatua ya serikali kuweka nguvu katika kuimarisha utendaji wa kazi takukuru ni wazi kilichopo ni kusubiri matokeo chanja kutokana na uwekezaji wa miundombinu ya majengo,na kuongeza rasilimali watu uweze kuleta matokeo chanja na tija kwa taifa.

Dec 3, 2025

TAWA WAPEWA MKAKATI USALAMA WA BINADAMU NA WANYAMAPORI

 WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII,DKT.ASHATU KIJAJI(MB) 

MAKALA MAALUM

 ZIARA YA   KIMKAKATI WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII MKOA WA MOROGORO

Na Thadei Hafigwa

 ILIKUWA ni ziara ya kimkakati  aliyoifanya  WAZIRI wa maliasili na Utalii,Dkt.Ashatu Kijaji(MB) ambapo ilitoa mwelekeo na maelekezo kwa mamlaka ya wasimamizi wa wanyamapori Tanzania(TAWA) kwa kutaja vipaumbele kwa kuzingatia  maagizo ya Rais wa Jamhuri Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan yaweze kutekelezwa kwa vitendo kwa masilahi ya nchi.

Waziri Kijaji amebainisha hayo mijini Novemba 24 Morogoro akiwa katika ziara yake ya kwanza toka ateuliwe kushika wadhifa huo katika kipindi cha pili cha awamu ya sita ya Rais Samia na kuongea na menejimenti ya TAWA,sanjari na kushiriki kwenye hafla ya kuzindua vitendea kazi kwa menejimenti na watumishi wa taasisi ya TAWA ambavyo ni magari 4,Pilipiki 33 na ndegenyuki ikiwa ni mkakati wa kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi wao.

Dkt.Kijaji alirejea hotuba aliyoitoa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan wakati akizindua bunge la 13 aliyoelekeza wizara ya maliasili na utalii na tasisi zake kuhakikisha wanaendelea kuimarisha ulinzi wa maeneo ya hifadhi na udhibiti wa wanyamapori na waharibifu dhidi ya mali na maisha ya wananchi.

Alisema kuwa,tayari serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan imeshaelekeza na kutoa nafasi ya kuajili watumishi na askari wa wanyamapori ili kwenda kuwahudumia wananchi na kupunguza kero dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yao.

”tunatakiwa tuendelee na ujenzi wa vituo vya ulinzi,tunatakiwa kuwa na mbinu za kisasa zaidi,na vifaa pia vya kisasa ikiwemo ndegenyuki,ambavyo tumezindua,tumizindua  magari,tumezindua pikipiki kwa hiyo hatuna visingizio tena kushindwa kuwahumia twendeni tukawadumie wananchi wetu”alisema.

“hivyo tunatakiwa kwenda kufanyakazi ya huduma kwa wananchi wetu  kwa kujali utu wao”

Waziri aliitaka menejimenti ya TAWA kujipanga katika kuhakikisha ya kuwa wanakwenda kutekeleza maelekezo hayo kwa weledi ili watanzania kuendelea kunufaika na rasilimali zao walizojaliwa na Mwenyezi mungu.

Aliwakumbusha kutambua kuwa msingi wa uwepo wa taasisi ya tawa ni  ulinzi wa wanyamapori bila ya kuwepo kwa jambo hilo hakutakuwemo kwa taasisi hiyo,hivyo wanapaswa  kuongeza ufanisi wa doria,itelejensia na matumizi ya teknolojia,ndegenyuki,kisukuma mawimbi,na vifaa rafiki vya ulinzi ili kulinda rasilimali muhimu zilizopo hapa nchini.

Aidha,mkakati mwingine alitaja ni kuzuia kwa kiwango cha juu vitendo vya ujangili ,uharibifu wa mazingira na biashara haramu za nyara ya serikali.

Waziri wa Maliasili na Utalii,Dkt Ashatu Kijaji(katikati) akikata utepe katika hafla ya uzinduzi wa vitendea kazi kwa maafisa wa wanyamapori mjini Morogoro alipofanya ziara ya kikazi,wengine walishiriki kushika utepe kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ta wanyamapori Tanzania(TAWA),Meja Jenerali Mstaafu,Hamis Semfuko,Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii,Hamad Chande,kutoka kushoto kwa Mhe.Waziri Kijaji ni Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA),Mlange Kabange

Pia,alihimiza kuendelea ushirikiano na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha maeneo yote chini ya tawa yanabaki salama na hakina anayeyachezea.

Suala lingine aliloliwekea kipaumbele ni kuhusisha mifumo ya taarifa,uchaguzi na tathmini ya matukio ili maamuzi ya kiutendaji yawe haraka,sahihi na yakiufanisi zaidi.

Alisisitiza na kuagiza kwamba hawatavumilia upotevu wa rasilimali za taifa,kwa kuwa Tawa wamewezeshwa kwa rasilimali  zote na utayari wa serikali ya awamu ya sita ni mkubwa katika kuhakikisha inaendelea kuweka mazingira  wezeshi ili kurahisha kutendaji kazi kwa urahisi zaidi.

Aidha,Waziri huyo wa maliasilia na utalii aliwataka tawa kuimarisha mapato na uendelevu wa taasisi kwa kujenga uwezo wa kifedha utakawezesha kulinda na kuendeleza maeneo yote walioaminiwa na kukabidhiwa na watanzania.

Alitoa maelekezo ya kuendelea kumaisha ukusanyaji wa mapato,kuhakikisha hakuna uvujaji na kuongeza ufanisi wa mifumo ya kifedha,ni muhimu sana mifumo ikasomana.

Aliweka mkazo kwa menejimenti ya tawa wa matumizi ya teknolojia katika ukusanyaji wa mapato ndani ya taasisi na kamwe kutoruhusu ukusanyaji wa fedha zikiwa mbichi,na kutumika zikiwa mbichi ili kuleta ufanisi na kurahisa kufanya tathimini kilichokusanya na kutumika katika mwaka uliopita.

Kadhalika aliwataka kuboresha fursa za uwekezaji rafiki hususan zenye tija katika mazingira yanayowazunguka katika maeneo ya utalii wa ekolojia kwa kuweka kambi za kitalii,utalii wa picha kwa kuonesha uwezo katika utendaji kazi.

Alihimiza menejimenti ya tawa kuongeza juhudi ya utangazaji wa vivutio vya utalii vilivyopo katika maeneo yote ya Tawa ili kuongeza idadi ya watalii wa ndani na nje,kwa ubunifu mbinu gani zitakazotumika katika kufanikisha jukumu hilo na kuibua vivutio vingine ili kufikia idadi ya watalii mil.8 kama ilivyoelekezwa katika ilani ya ccm 2025-2030.

“ni wazi tukafahamu bila ya  mapato hakuna maendeleo uendelevu wa taasisi yetu wala ya taifa letu,moja ya taasisi zinazotakiwa kuongeza mapato ni pamoja na taasisi yetu(tawa)”alisema

Alisema kila mmoja  alimsikia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia kwamba kipindi hiki ni cha kutumia rasilimali zilizopo hapa nchini,kutumia mapato ya ndani ili kuweza kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo nchini.

Suala lingine alilosisitiza ni utoaji wa huduma kwa wananchi ni lazima ziweze kuzingatia utu,kwamba dhamira ya serikali ni kuwatumia watu kwa utu,heshima na haki,hivyo migongano katika ya watu na wanyamapori ishughulikiwe kwa haraka kwa kutumia uadilifu,weledi na vifaa na miundombinu ilivyopo katika kuwahudumia wananchi kwenye maeneo yao.

Alikemea tabia walionayo baadhi ya watumishi wa tawa ya kuwataka wananchi kuchangia gharama za mafuta.

“ipo tabia ya kuwaambia wananchi,kama unataka nije changia mafuta,jambo hilo halipo na katibu mkuu hili naomba ulisimamie ,mwananchi hatakiwi kuchangia mafuta ili askari wetu akifikie mwananchi,ipo tabia kwa baadhi ya maeneo.”alisema

Awali,Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA),Mlange Kabange,asema wapo tayari kuteleza maagizo yote yanayotolewa na serikali katika kuhakikisha malengo ya kuwahudumia wananchi yanafikiwa kikamilifu katika uhifadhi wa wanyamapori.

Kabange anasema kuwa tawa inajukumu la kusimamia mapori ya nje ya Tanapa na  Ngorongoro,wanasimamia mapori ya akiba 28,na mapori tengevu 23,yote kwa pamoja yana ukubwa wa kilometa za mraba 133,276.36,eneo hilo ni kubwa zinazidi ukubwa wa baadhi ya nchi.

Alisema kuwa tawa wanatambua kuwa wana jukumu la kuhakikisha rasilimali za wanyamapori  zinalindwa na kwamba wafanikio wanayopata yanatokana na serikali ya awali ya sita imekuwa ikiwapatia fedha za kuteleza bajeti zao kwa asilimia 100 kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Alisema mbali ya fedha za bajeti,Rais Samia aliwapatia fedha za kuboresha miundombinu za utalii,katika kipindi cha oviko sekta nyingi zilitetereka, lakini tawa walipewa fedha bil 12.9 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya utalii.

Sanjari na hayo,alisema kuwa maafisa na watumishi wa tawa waliongezewa mshahara na watumishi 3000 wenye sifa walipandishwa vyeo jambo ambalo ni rekodi ambayo haijawahi kutokea toka kuasisiwa kwa tawa.

Aliishukuru serikali kupitia Rais Samia kuwa sekta ya utalii imekuwa kutokana na filamu ya royal tour na kupelekea mwaka jana (2024) walipata kampuni ya uwekezaji kutoka china katika sekta ya utalii,jambo ambalo siku za nyuma halijawahi kutokea.

Aidha,alishukuru wizara ya maliasili na utalii kwa kuandaa miongozo,sera na kanuni zinazowarahishia taasisi kutekeleza majukumu yake sekta ya utalii wa uwindaji na utalii wa picha.

Naye,Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ta wanyamapori Tanzania(TAWA),Meja Jenerali Mstaafu,Hamis Semfuko alimpongeza Rais Samia kwa kupata ridhaa ya kuongeza taifa la Tanzania kwa kipindi cha pili cha awali ya sita,ambapo inatokana na imani waliokuwa nayo wananchi kwake na uchapakazi wake katika sekta mbalimbali.

Meja Jenerali Mstaafu Semfuko pia alionesha shukrani zake kwa serikali kwa kuweka mazingira wezeshi katika utekelezaji wa majukumu ya tawa katika ulinzi na uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake.

 Kwa upande wake Katibu wa Wizara ya Maliasili na Utalii,Dkt.Hassan Abbas alisema ziara waliifanya ni kutembelea jeshi la uhifadhi kujua kazi zinafanyika,mafanikio na changamoto zilizopo kwa wananchi wanaishi karibu na maeneo ya hifadhi na namna ya kukabiliana nazo.

Dkt. Abbas ametaja Tanzania inaongoza kuwa na simba wengi duniani wapatao 17,000,jumla ya chui 24,000 ambapo Tanzania inaongoza Afrika na duniani,huku idadi ya ni nyati 200,025,na tembo 60,000.

Sep 20, 2025

MGOMBEA UBUNGE ATOA MATUMAINI MAPYA KWA WANANCHI MOROGORO KUSINI

Mgombea ubunge Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume

Na Thadei Hafigwa

WANANCHI wa Jimbo la Morogoro Kusini wameanisha kero na kuziwasilisha kwa Mgombea ubunge kwa tiketi cha chama cha Mapinduzi,Zuberi Mfaume ili zipatiwe ufumbuzi ikiwemo changamoto za miundombinu ya barabara,maji, uchungaji holela wa mifugo ilinayoharibu mazao ya wakulima shambani husuan kipindi cha kilimo.

Wakazi wa Kata ya Selembala,Kisaki,Mvuha,Mngazi na Bwakila chini Morogoro vijijini wamebainisha hayo kwa nyakati tofauti kwenye mikutano kampeni inayoendelea jimboni humo ambapo wameonesha imani walionayo Mgombea ubunge wa ccm jimbo la Morogoro kusinijambo lililowalazimu wagombea wengine kutoka vyama vingine vya kisiasa walionesha nia ya kuwania nafasi ya ubunge wa jimbo hilo  kutorudisha fomu walizochukua tume huru ya taifa ya uchaguzi.

Zuberi Mfaume ni Mgombea pekee ubunge Jimbo la Morogoro kusini kwa tiketi ya CCM ambaye Oktoba 29, 2025 siku ya Kupiga kura atapigia kura ya Ndiyo au Hapana kwenye kinyang’anyiro hicho.

Wagombea nafasi ya udiwani na Mgombea Ubunge,Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume wakiwa katika picha ya pamoja baadhi ya viongozi wa ccm wilaya ya Morogoro vijijini,mara baada ya kumaliza harakati za kunadi Ilani ya CCM 

Mfaume akiwa katika mikutano yake ya kampeni katika kata ya Selembala,Mvuha,Kisaki,Mngazi na Bwakila Juu, amejitwika mzigo wa changamoto zinazowakabili wananchi wa  maeneo hayo ambazo ni miundombinu ya barabara,uchungaji holela wa mifugo ambayo inaharibu mazao ya wakulima,stakabadhi ghalani pamoja na pungufu wa maji katika maeneo ya vijijini ambayo kwa mujibu wa sera ya maji,inayoelekeza wakazi wa vijijini wanapaswa kufikiwa huduma ya usambazaji wa maji kwa asilimia 85.

amewahakikishia wananchi wa maeneo hayo kuwa changamoto zinazowakabili zitashughulikiwa mara  baada ya kuchaguliwa kuhudumu nafasi ya ubunge kwa kuwa tayari ashaandaa mkakati maalum wa kuzipatia ufumbuzi changamoto zilinazowakabili  wananchi,.

“kipaumbele changu cha kwanza nitaimarisha ofisi ya mbunge kwa kuweka  dawati la msaada wa sheria ili kuwasaidia wananchi kukabiliana na changamoto za kisheria”alisema.

Mgombea huyo mbali na taaluma nyingine alizonazo pia ni mwanasheria, alinukuu ahadi iliyoanishwa kwenye Ilani ya CCM 2025-2030 iliyoelezea utatuaji wa changamoto ya miundombinu ya barabara kutoka ubenazomozi hadi Mvuha.

“ahadi namba 265 katika Kitabu cha Ilani ya chama cha Mapinduzi unasomeka Mradi wa upembuzi yakinifu katika barabara ya Ubenazomozi, Ngerengere, kuelekea kituo cha SGR,Tununguo,Selembala,Mvuha inaungana na Bigwa Kisaki kuelekea bwawa la Mwalimu Nyerere itajengwa katika kiwango cha lami”.

Harakati za kampeni zinapopamba moto viongozi wa ccm wakipongezana na Mgombea ubunge wa Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume

Rajabu Changa ni wakili msomi wa Mahakama kuu Tanzania, katika maoni yake ameshauri namna ya kutatua migogoro mingi iliyopo katika maeneo ya vijijini inatokana na kukosekana kwa uwelewa katika masuala ya sheria hususan sheria ya Ardhi na.4 ya mwaka 1999 na sheria ya KIjiji na.5 ya mwaka 1999.

“pamoja kutambua sheria hiyo ya ardhi na vijiji katika kutatua changamoto za migogoro ya ardhi inapaswa wanakijiji kuunda sheria ndogondogo na kutambua Sheria ya serikali za Mitaa,Mamlaka ya Wilaya,Sura 287 toleo la mwaka 2023,kwamba kifungu  cha 170 kinaeleza Mamlaka ya serikali ya Kijiji kutunga sheria zake,village by laws”alisema.

Alibainisha ya kuwa,Kata ya Selembala imeingizwa katika barabara kuu inayotoka Ubenazomozi mpaka  Mvuha ambayo tayari imeingizwa katika upembuzi yakinifu ili ijengwe kwa kiwango cha rami,kwamba imetafsiriwa kama barabara kuu kuelekea katika bwawa kubwa la kufufua umeme,Bwawa la Nyerere.

Pia, Mgombea Ubunge Jimbo la Morogoro Kusini ameahidi kushughulikia changamoto ya miundombinu ya barabara kutoka eneo la getini hadi Kijiji cha Kiganila kilichopo kata Selembala kwa kutumia mfuko wa jimbo.

“ninataka kuwaahidi kwamba serikali ya Chama Cha Mapinduzi ilitenga fedha maalum ya mfuko wa jimbo,moja ya kazi zake ni kutatua changamoto kama hizi,nitakuja kuwashukuru,tutakaa pamoja na tutaona namna gani tutapitisha greda walau barabara yetu iweze kupitika”alisema.

Kikosi kazi cha Chama cha Mapinduzi wakiwa na Mgombea ubunge wa Jimbo la Morogoro Kusini,Zuberi Mfaume wapili kutoka kushoto aliyevaa shati la Kijani mwenye miwani

Aidha,alianisha changamoto nyingine ni changamoto ya vijiji viwili Bwilachini na Kibulumo vilipitiwa na mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere toka mwaka 2019 wananchi wa vijiji hivyo hawana uongozi baada ya kupatiwa eneo lingine la kuishi, la mjipya.

Mzee Zuberi Mwenegoha diwani mstaafu wa Kata ya Selembala anasema kwa sasa wananchi wanasubiri maelekezo ya uongozi wa CCM Mkoa wa Morogoro ambao wameahidi kulishughulikia suala hilo.

“kwa sasa tunasubiri uongozi wa chama cha mapinduzi Mkoa wa Morogoro ambao wameahidi kuja kututembelea na kusikiliza kero zetu ili zipatiwe ufumbuzi kwa kuwa ndicho chama chenye dola”alisema Mzee Mwenegoha.

Katika mikutano yake amekuwa alitoa elimu ya sheria umuhimu wa kuishi bila ya kubaguana kati ya wakulima na wafugaji akinukuu katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.ibara ya 13(1).

“Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki,bila ya ubaguzi wowote,kulindwa na kupata haki awa mbele ya sheria.”

Hoja hiyo imekuja baada ya wananchi kuelezea kero walionayo ya mifugo kuingia kwenye mashamba ya wakulima na kuharibu mazao. “Mkulima hana haki ya kuugua mifugo ya wafugaji,wala mfugaji hana haki ya kuingiza mifugo yake kwenye mashamba ya wakulima na kuharibu mazao.”alisema.

Aliwaahidi wananchi kumwamini kero zinazowatatiza zitawekewa utaratibu maalum wa kuzishughulikia sanjaria na kuzingatia sheria za nchi bila ya kumuonea mtu yeyote.

Temotheo Tapo kutoka jamii ya wafugaji mkazi wa  Kijiji cha Mgogoni,Kata ya Selembala amesema baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo kwenye mashamba ya watu na kuharibu mazao si jambo jema,hata hivyo aliomba serikali kuhakikisha wanawawekea mazingira mazuri ya kujengea malambo yakunyweshea mifugo.

“Mifugo yetu inakosa maji,serikali imetukataza kutumia maji ya mito kunyweshea mifugo yetu.mifugo yetu pia inakabiliwa na magonjwa ya mapafu,midomo na miguu kuvimba tunahitaji majosho”alisema Tapo.

Katika ziara ya Kampeni Zuberi alimbatana na viongozi mbalimbali wa chama,Katibu wa Vijana wa Wilaya ya Morogoro vijijini,Mussa Idowa,wajumbe  wa Kamati ya Siasa Wilaya ya Morogoro vijijini, Donny Mbena,Zamoyoni Zuberi, Scolastika Salum,Katibu wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Morogoro, na Hamza Yahya mjumbe wa halmashauri kuu CCM  Mkoa wa Morogoro.

 Kwa nyakati tofauti walinadi wagombea kwenye mikutano ya kampeni ili kuhakikisha wananchi wanajitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura na wanachagua wagombea wanaotokana na chama cha mapinduzi,Samia Suluhu Hassan katika nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Zuberi Mfaume nafasi ya ubunge pamoja na madiwani wanaogombea katika kata 17 zilizopo kwenye Jimbo la Morogoro kusini.

Kwa upande wake Mjumbe wa halmashauri kuu ccm Mkoa wa Morogoro,Hamza Yahya aliwahimiza wanachama na wapenzi wa chama hicho kuhakikisha wanawahamasisha wananchi wengine wenye sifa ya kupiga kura wanajitokeza na kukipigia kura chama cha mapinduzi ili falsafa ya mafiga matatu iweze kutekelezeka kwa vitendo,kwa kuzingatia mnyororo wa uwajibikaji wa pamoja.

Jimbo la Morogoro kusini lina jumla ya kata 17 ambazo ni Mtombozi,Selembala,Bungu,Mvuha,Kisemo,Kasanga,Konde,Lundi,Kibuko,Kolero,Tawa,Kibogwa,Bwakira chini,Kisaki,Mngazi, Bwakila juu na Singisa.

Aug 15, 2025

WANAHABARI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA SHERIA

 WANAHABARI WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA SHERIA

Mwezeshaji wa mafunzo,Peter Kimath akiwasilisha mada ya usalama mitandaoni kwa wanachama wa MoroPC
Na Mwandishi wetu

WAANDISHI wahabari wametakiwa kufanya kazi kwa kuzingatia sheria ili kuepuka kuingia kwenye migogoro wakati wa kuripoti habari kuelekea katika kipindi cha uchaguzi mkuu Oktoba 2025.

Peter Kimath,Elizabeth Tanzania na Peter Laurence ni wakufunzi waliojengewa uwezo na UTPC kwa kushirikiana na IMS kwa lengo la kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari sanjari na usalama mtandaoni na masuala ya saikolojia ya maisha kwa waandishi wa habari.

Peter Kimath amesema msingi bora wa mwandishi kufanya kazi zake vizuri bila kuingia kwenye changamoto ni kufuata sheria zinazomuongoza,kufuata sheria za nchi na kuangalia sera za chombo anachofanyia kazi kwa lengo la kulisha walaji wake kile wanachotegemea

“tunapaswa kuelewa sheria na kanuni zinazohusu uchaguzi na vyombo vya habari, kama Sheria ya Huduma za Habari (2016), Sheria ya Makosa ya Mtandao (2015) na Kanuni za Tume ya Uchaguzi.”anasema Kimath.

Halfan Diyu ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo akichangia mada

Mwandishi Nguli,Halfan Diyu anasema mafunzo haya yamekuja wakati muafaka kwani yamewakumbusha vitu vingi muhimu vya kuzingatia wakati wa kuripori habari za uchaguzi na nyingine katika jamii.

“tunaishukuru UTPC na IMS  kwa kuona umuhimu wa mafunzo haya kwetu,naamini tutayatumia vizuri katika kuripoti habari,na kufuata maadili ya kiuandishi ili kuepuka kuingia kwenye msigano.

Hamida Shariff ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo anasema kutokana na teknolojia vitu vinabadilika kila siku katika tasnia ya habari,hivyo wanahabari wanapaswa kukumbushwa kila wakati katika masuala mbalimbali ikiwemo ulinzi wa taarifa binafsi na sheria zinawaongoza.

“nimejifunza vitu vizuri vitakavyonisaidia katika utendaji wangu wa kazi kila siku ikiwemo,namna ya kulinda vifaa vyangu vya kazi,kujilinda wakati wa kuripoti habari uchunguzi,UTPC nawaomba kuendelea kutoa mafunzo kama haya kwani bado wanahabari tunachangamoto nyingi zinahitaji kutatuliwa kwa njia ya kupewa elimu".

Aug 14, 2025

WANAHABARI MOROGORO WAPEWA MAFUNZO KUFANYAKAZI KWA WELEDI

 WANAHABARI MOROGORO WAPEWA MAFUNZO KUFANYAKAZI KWA WELEDI 

Baadhi ya washiriki na wanachama wa MoroPc wakifuatilia kwa umakini mafunzo yalioandaliwa na UTPC kwa kushirikana na IMS.

Na Mwandishi wetu

WANAHABARI wametakiwa kuhakikisha Wanafanya kazi kwa uhuru bila hofu ya kudhuriwa.Wanalindwa dhidi ya unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia au kisheria.

Peter Laurence,Elizabeth Tanzania na Peter Kimath ni wakufunzi waliojengewa uwezo na UTPC kwa kushirikiana na IMS kwa lengo la kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari sanjari na usalama mtandaoni na masuala ya saikolojia ya maisha kwa waandishi wa habari.

Laurence alisema waandishi wa habari wanapaswa kuongeza umakini wanapotumia mitandao ya kijamii wakati wanapotimiza wajibu wao,kwani kutawaweka salama na kuepuka kudukuliwa kazi zao.

Peter Kimath alisema kuwa waandishi wa habari wanapaswa kupewa mazingira salama ya kufanya kazi, hasa wakati wa kuripoti katika maeneo hatarishi (kama maandamano, migogoro ya kisiasa, au vita).

Mwezeshaji Peter Laurence aliwasilisha mada huku wanachama wa Moropc walifuatilia kwa karibu.

Kimath akiwasilisha mada kwa waandishi wa habari wa Morogoro kuhusu ulinzi na usalama kwa waandishi wa habari alisema waandishi wa habari wazingatie weledi wanapotimiza wajibu wapo,pia wanapokabiliwa na changamoto na kadhia katika mazingira ya kazi,ambayo yanaviashiria hatarishi wawasiliane na viongozi wa Klabu za waandishi.

Mada ya saikolojia ya maisha katika mazingira ya waandishi wa habari iliwasilishwa na Elizabeth Tanzania ambaye aliwakumbusha waandishi wa habari kutambua jinsi athari ya Trauma (Kiwewe) na namna ya kukabiliana nayo.

Aliwaeleza waandishi wanapaswa kutambua maana ya trauma wa kuielezea kuwa ni hali ya maumivu makubwa ya kihisia au kiakili yanayosababishwa na tukio la kushtua sana, kama kubakwa, ajali mbaya, au kushuhudia vifo. Hali hii huweza kuathiri maisha ya mtu kwa muda mrefu.

Elizabeth Tanzania,Mwezeshaji akiwa makini katika kuwasilisha mada kwa waandishi na wanachamawa Morogoro.

“dalili ya trauma ni kumbukumbu mbaya zinazojirudia (flashbacks), kujitenga na watu, hofu au mshangao kupita kiasi,Kutojiamini, na kukosa usingizi”

Jul 27, 2025

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

 NAIBU KATIBU MKUU WA WIZARA YA ELIMU,SAYANSI NA TEKNOLOJIA,DK.HUSSEIN OMARY AKISISITIZA JAMBO.

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

WALIMU zaidi 5000 wa shule za sekondari hapa nchini kutoka kanda 7 wamenufaika na mafunzo ya  TEHAMA katika kipindi cha miaka mitatu, ambapo kwa mwaka huu pekee, walimu 1,870 wameshiriki mafunzo hayo yaliyofanyika katika vituo vya Tukuyu - Mbeya na Chuo cha Ualimu Morogoro kutokana na uwekezaji uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk.Samia Suluhu Hassan

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward Wawa alibanisha hayo katika mjini Morogoro katika hafla ya kufunga mafunzo ya awamu ya tatu kwa walimu kutoka mikoa ya Morogoro,Pwani,Dar es Saalam,Lindi na Mtwara.

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward akiwasilisha taarifa yake kwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia,Dk.Hussein Omary.

Wawa alisema kuwa kuwa serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeanza kutekeleza mradi wa kuboresha elimu ya sekondari kwa kuimarisha ujuzi wa walimu kupitia mafunzo ya TEHAMA  toka mwaka 2022 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kiashiria na 9 cha mradi wa matokeo makubwa kinacholenga kuwajengea walimu uwezo wa kufundisha kwa kutumia mbinu za kisasa na vifaa vya kidijitali.

Mafunzo hayo yametekelezwa kwa awamu tatu,kwa kuzingatia kanda 7 zilizopo,katika awamu ya kwanza,iliyofanyika mwaka 2022/2023,walimu 500 kutoka kanda ya kati na kanda ya kaskazini,walipatiwa mafunzo hayo.

“Awamu ya pili yalifanyika mwaka 2023/2024 ambapo walimu 2632 kutoka kanda ya Ziwa,kanda ya magharibi,kanda ya kaskazini na kanda ya kati,walipatiwa mafunzo”alisema.

Baadhi ya Walimu Washiriki wa mafunzo ya Tehama mjini Morogoro walifuatilia kwa umakini Hotuba ya Mgeni Rasmi,Naibu Katibu Mkuu,Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Dk.Hussein Omary (hayupo pichani) kwenye hafla ya kufunga mafunzo hayo yaliofanyika katika Chuo cha Ualimu,Morogoro.

Aidha,alifafanua kuwa awamu ya tatu ya mafunzo kwa walimu wa Tehama yamefanyika katika mwaka 2024/2025 kwa kuhusisha vituo viwili,kituo cha kwanza Tukuyu Mbeya yalianza Julai 14-18,2025 na kuwanufaisha walimu 941,na Morogoroo ambapo jumla ya walimu 929 wamenufaika na mafunzo hayo.

Mgeni Rasmi wa hafla hiyo ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Hussein Omary, ambapo ametoa wito kwa walimu nchini kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo ya kitaaluma kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, akisisitiza kuwa elimu jumuishi na yenye usawa ni msingi wa maendeleo endelevu ya taifa.

Dk. Hussein alisema kuwa serikali ina dhamira ya dhati ya kuwekeza kwa walimu ili kuimarisha elimu bora inayomfikia kila mtoto, bila kujali mahali alipo,wizara yake inaendelea kutekeleza sera ya elimu kwa vitendo, kwa kuweka mkazo katika mitaala, miundombinu, TEHAMA na maendeleo ya walimu ili kuhakikisha maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Sami Suluhu Hassan yanatimia.

“Mafunzo haya ni tafsiri ya maono ya Mheshimiwa Rais. Tunatekeleza kwa vitendo sera ya elimu jumuishi na bora. Lengo ni kuhakikisha kila mtoto anapata elimu sawa,bila kujali eneo analotoka,” alieleza.

Dk. Hussein alisisitiza nafasi ya walimu kama nguzo kuu ya mabadiliko katika mfumo wa elimu nchini, akisema mafanikio ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji wa kweli kwa walimu.

Baadhi ya washiriki wa hafla ya kufunga mafunzo kwa walimu wa sekondari juu ya TEHAMA,Mjini Morogoro

Aidha, alibainisha kuwa serikali imeanza kuimarisha miundombinu ya kufundishia kwa kutumia TEHAMA ili kukabiliana na changamoto za karne ya 21, huku akiwataka walimu kuwa mfano kwa jamii kwa kuonyesha weledi, maadili na ubunifu katika kazi zao.

Mafunzo hayo yamewahusisha walimu kutoka shule mbalimbali nchini yakiwa na malengo kuwajengea uwezo kwa kutumia vifaa na rasilimali za Tehama  darasani,kuongeza ubora wa utoaji wa elimu kupitia mbinu shirikishi za kidigitali,kuimarisha matokeo ya ufundishaji kwa wanafunzi kupitia teknolojia.