MWANAMKE MOROGORO MBARONI KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA MUMEWE
Na Thadei Hafigwa
JESHI la Polisi mkoa wa Morogoro limemtia mbaroni,Mwanamke Jobita Bategeuye Budyo(30) mkazi wa Maafisa,Manispaa ya Morogoro kwa tuhuma ya mauji ya mume Abeli Charles(44) kwa kile kinachodaiwa ni kutokana na mapenzi.
inaelezwa kuwa kabla ya kifo kulitokea kama mabishano ya wanandoa wakati wa maandalizi ya chakula,
Kutokana na hali hiyo ikasababisha tukio la kusikitisha baada ya mwanaume mwenye umri wa miaka 44 kupoteza maisha katika mazingira yanayodaiwa kuhusishwa na mgogoro wa kifamilia katika eneo la Mafisa, Manispaa ya Morogoro.
Abeli Charles wakati wa uhai wake,alikuwa. ni mfanyabiashara, huku mtuhumiwa akitajwa kuwa ni fundi cherehani na mkazi wa eneo hilo.
Tukio hilo linadaiwa kutokea usiku wa Agosti 31, 2026, nyumbani kwa wanandoa hao, baada ya mazungumzo yao kubadilika na kuwa mabishano makali yaliyodaiwa kuhusishwa na masuala ya unyumba.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, ACP Andrew Kantimbo, mabishano hayo yaligeuka kuwa ugomvi, ambao baadaye ulipelekea Abeli Charles kupata majeraha makubwa katika maeneo ya shingoni na kichwani na kusababisha kifo chake.
Kamanda Kantimbo amesema, kwa mujibu wa taarifa za awali za uchunguzi, mtuhumiwa anadaiwa kutumia kitu chenye ncha kali kumshambulia na kumjeruhi marehemu, ambaye baadaye alipoteza maisha kutokana na majeraha aliyoyapata.
“Chanzo cha awali cha tukio hilo kinahusishwa na mgogoro wa kifamilia unaodaiwa kuchochewa na masuala ya unyumba,” amesema Kamanda Kantimbo, huku akibainisha kuwa uchunguzi wa kina unaendelea kubaini mazingira yote ya tukio hilo.
Jeshi la Polisi linamshikilia Jovita kwa ajili ya uchunguzi zaidi kabla ya kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria kulingana na matokeo ya uchunguzi.
Tukio hilo limeibua tena mjadala kuhusu namna migogoro ya kifamilia inavyoweza kugeuka kuwa matukio ya ukatili pale ambapo wahusika wanashindwa kutumia mazungumzo, uvumilivu na njia nyingine za amani kutatua tofauti zao.
Kamanda Kantimbo ametoa wito kwa wanandoa na familia kwa ujumla kuepuka matumizi ya nguvu katika kushughulikia migogoro, akisisitiza umuhimu wa kutafuta msaada kutoka kwa ndugu, viongozi wa jamii, viongozi wa dini au mamlaka nyingine zinazohusika kabla ya migogoro kufikia hatua ya kuhatarisha maisha.
Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa kwa wakati kuhusu matukio ya ukatili na viashiria vya migogoro inayoweza kuhatarisha usalama wa watu.
Amesema ushirikiano wa jamii ni muhimu katika kuzuia matukio ya uhalifu na kulinda makundi yaliyo katika mazingira hatarishi, yakiwemo wanawake, watoto, wazee na watu wenye ulemavu.


















































