Na Thadei Hafigwa, Morogoro
SERIKALI ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha misingi ya utawala bora, uwajibikaji na mapambano dhidi ya rushwa kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Hatua hiyo imejidhihirisha kwa uzinduzi wa jengo jipya la Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Morogoro lililogharimu Shilingi bilioni 1.627, mradi unaotarajiwa kuongeza ufanisi wa watumishi, kuboresha utoaji wa huduma na kusogeza karibu zaidi huduma za taasisi hiyo kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa jengo hilo uliofanyika Juni 1, 2026 mjini Morogoro, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha taasisi zinazosimamia uwajibikaji zinakuwa na mazingira bora ya kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
MUONEKANO WA JENGO LA OFISI YA TAKUKURU MKOA WA MOROGORO
“Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuwekeza katika kuimarisha taasisi za mapambano dhidi ya rushwa ili ziweze kutekeleza wajibu wake kwa weledi na kwa kiwango kinachokidhi matarajio ya wananchi,” alisema Chalamila.
Alieleza kuwa TAKUKURU kwa sasa ina ofisi 145 nchini, zikiwemo ofisi za mikoa 28, wilaya 111 na vituo maalumu sita, huku ofisi 70 pekee zikiwa zinamilikiwa na taasisi hiyo na nyingine zikiendelea kujengwa kulingana na upatikanaji wa fedha za Serikali.
Kwa mujibu wa Chalamila, katika mwaka wa fedha 2025/2026 taasisi hiyo inaendelea na ujenzi wa majengo 11 mapya, yakiwemo ya mkoa mmoja na wilaya 10, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuondoa changamoto ya uhaba wa majengo ya ofisi nchini.
MKURUGENZI MKUU WA TAKUKURU, BW. CRISPIN FRANCIS CHALAMILA,AKISHIRIKIANA NA MKUU WA WILAYA YA MVOMERO,MAULID DOTTO AMBAYE ALIMWAKILISHA MKUU WA MKOA WA MOROGORO,ADAM MALIMA KATIKA HAFLA YA UZINDUZI WA JENGO LA OFISI YA TAKUKURU MKOA WA MROGORO.
“Bado tuna ofisi 64 ambazo hazina majengo ya kudumu. Hivyo, kukamilika kwa jengo la Morogoro ni hatua muhimu katika safari ya kuimarisha uwezo wa taasisi yetu kufikia wananchi kwa karibu zaidi,” alisema.
Taarifa ya utekelezaji wa mradi iliyosomwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Usimamizi wa Milki wa TAKUKURU, Eng. Dk. Emmanuel Kiyabo, ilieleza kuwa mradi huo ulianza Machi 6, 2025 kwa bajeti ya Shilingi 1,600,016,922.08 na kukamilika Machi 30, 2026 baada ya kuchelewa kwa takribani miezi mitatu kutokana na changamoto mbalimbali za utekelezaji.
Miongoni mwa changamoto zilizochelewesha mradi huo ni ucheleweshwaji wa vifaa vya ujenzi hususan mabati, uhaba wa baadhi ya vifaa maalumu vya ukuta wa vioo, mvua za masika pamoja na kusitishwa kwa shughuli mbalimbali kufuatia mazingira ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
Mradi huo ulitekelezwa kwa mfumo wa “Design and Build” kwa ushirikiano kati ya TAKUKURU na Shirika la Magereza (PCS), ambapo wataalamu wa taasisi hizo walishirikiana katika usanifu na ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya kisasa.
MKURUGENZI MKUU WA TAKUKURU, BW. CRISPIN FRANCIS CHALAMILA AKIMWAGILIA MTI MAJI, BAADA YA KUPANDA MOJA YA KIASHIRIA YA UZINDUZI WA JENGO LA TAKUKURU MKOA WA MOROGORO.Jengo hilo la ghorofa moja lina eneo la sakafu lenye mita za mraba 575 na limejumuisha nyumba ya walinzi, nyumba ya mfumo wa umeme na jenereta, uzio wa kisasa wenye mageti yanayotumia mfumo wa umeme, tenki la maji la chini lenye uwezo wa kuhifadhi lita 60,000 pamoja na mnara wa matenki ya maji.
Chalamila alisema gharama za mradi ziliongezeka kwa asilimia 1.74 pekee kutoka bajeti ya awali, jambo ambalo linaonesha usimamizi mzuri wa fedha za umma katika utekelezaji wa mradi huo. Ongezeko hilo lilitokana na maboresho yaliyofanyika wakati wa utekelezaji ikiwemo kuongeza mifumo ya mageti ya umeme na kupanua eneo la paving blocks.
Mbali na uwekezaji wa miundombinu, Chalamila alisisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kusimamia matumizi ya fedha za umma na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana.
Alisema uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi ni nguzo muhimu katika kuzuia mianya ya rushwa na kujenga imani kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya rasilimali za Taifa.
Katika hatua nyingine, aliwataka watumishi wa TAKUKURU kuyatunza majengo na vifaa vinavyotolewa na Serikali ili viweze kudumu kwa muda mrefu na kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
Pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika maadili kwa vijana kupitia Klabu za Wapinga Rushwa mashuleni, akisema kuwa mapambano dhidi ya rushwa hayawezi kufanikiwa bila kujenga kizazi chenye uadilifu, uzalendo na uwajibikaji.
Aliwataka viongozi wa dini, vyama vya siasa, asasi za kiraia na wananchi kwa ujumla kushirikiana na TAKUKURU katika kuelimisha jamii kuhusu madhara ya rushwa na kuhamasisha utamaduni wa kukataa na kuripoti vitendo vya rushwa.
“Mapambano dhidi ya rushwa ni jukumu la kila Mtanzania. Ushirikiano wa wananchi ndiyo silaha kubwa katika kujenga taifa lenye uwajibikaji, haki na maendeleo endelevu,” alisema.
Uzinduzi wa jengo hilo unatajwa kuwa sehemu ya juhudi pana za Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha taasisi za umma, kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma na kuendeleza vita dhidi ya rushwa kama msingi wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.




















.jpg)









