SERIKALI YAWEKA MKAKATI WA FEDHA, MIUNDOMBINU KUCHOCHEA UCHUMI NYANDA ZA JUU KUSINI
Na Mwandishi wetu
SERIKALI imeweka mkakati wa kuhakikisha upatikanaji wa fedha za
miradi ya miundombinu unakuwa wa uhakika, hatua inayolenga kuharakisha
utekelezaji wa miradi ya barabara na miundombinu mingine muhimu kwa ajili ya
kuchochea shughuli za uzalishaji na ukuaji wa uchumi nchini.
Mkakati huo unalenga zaidi
kuimarisha miundombinu katika maeneo ya uzalishaji, hususan Kanda ya Nyanda za
Juu Kusini, ambayo ni miongoni mwa maeneo muhimu kwa uzalishaji wa chai na
mazao mbalimbali ya kilimo.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar
(Mb), aliyasema hayo
alipofika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya wakati wa kuhitimisha sherehe
za Maadhimisho ya Nane-Nane yaliyofanyika katika Viwanja vya John Mwakangale,
jijini Mbeya.
Alisema Serikali imejipanga
kuhakikisha fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo zinapatikana kwa wakati ili
kuondoa changamoto ya kuchelewa kwa utekelezaji wa miradi, hasa ya barabara na
miundombinu mingine inayochochea shughuli za kiuchumi.
Kwa mujibu wa Waziri huyo,
kwa muda mrefu utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo ulikuwa ukikabiliwa
na changamoto ya ucheleweshaji wa fedha, hali iliyosababisha miradi kadhaa
kusuasua.
Hata hivyo, alisema Serikali
imefanya mageuzi ya kimfumo kwa kuweka utaratibu wa kuhakikisha asilimia 70 ya
mapato yanayokusanywa kupitia mifuko maalum yanaelekezwa moja kwa moja kwenye
mifuko hiyo badala ya kupitia Hazina.
“Katika mwezi wa Julai pekee,
jumla ya shilingi bilioni 324 zilitolewa kwa mifuko mbalimbali ya maendeleo,
ambapo shilingi bilioni 76 zilipelekwa moja kwa moja kwenye Mfuko wa Barabara.
Utaratibu huu utaendelea kwa mwaka mzima wa fedha ili kuhakikisha miradi ya
miundombinu haikwamishwi na uhaba wa fedha,” alisema Mhe. Balozi Omar.
Balozi Omar alisema Serikali pia inaendelea kushirikiana na sekta ya fedha kutafuta njia mbadala za kupata fedha nyingi kwa wakati kwa ajili ya kugharamia miradi mikubwa ya miundombinu.
Alisema miongoni mwa njia
zinazotazamwa ni matumizi ya hati fungani za miundombinu (infrastructure bonds), ambazo zinaweza kusaidia kupata fedha
za miradi mikubwa mapema badala ya kusubiri mapato ya ndani kukusanywa hatua
kwa hatua.
Kwa mujibu wake, hatua hiyo
itasaidia Serikali kuharakisha utekelezaji wa miradi yenye umuhimu mkubwa kwa
uchumi na wananchi.
Akizungumzia umuhimu wa
miundombinu, Balozi Omar alisema barabara ni kiungo muhimu kati ya maeneo ya
uzalishaji, masoko na viwanda, hivyo uwekezaji katika sekta hiyo una nafasi
kubwa katika kuongeza tija na kipato cha wananchi.
Alisema hali hiyo ni muhimu
zaidi katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, ambako kilimo cha chai na mazao
mengine kinafanyika kwa kiwango kikubwa.
“Maeneo haya ya Nyanda za Juu
Kusini, ambako zao la chai na mazao mengine ya kilimo huzalishwa kwa wingi,
miundombinu bora ya barabara itasaidia kuongeza tija kwa wakulima na kuchochea
ukuaji wa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao hayo,” alisema.
Aliongeza kuwa miundombinu
bora itarahisisha usafirishaji wa mazao, kupunguza gharama za usafirishaji na
upotevu wa bidhaa, pamoja na kufungua fursa za masoko mapya kwa wakulima na
wazalishaji.
“Hii ndiyo njia ya kuongeza
kipato cha wakulima na kukuza uchumi wa nchi,” alisema.
Balozi Omar pia alisisitiza
umuhimu wa kuimarisha usimamizi wa miradi ya miundombinu ili kuhakikisha
wakandarasi wanatekeleza majukumu
Alisema wakandarasi
watakaobainika kuchelewesha utekelezaji wa miradi bila sababu za msingi
watachukuliwa hatua kali, ikiwemo kuwekwa kwenye orodha ya kutopatiwa zabuni
nyingine za Serikali.
Alisisitiza kuwa suala la
miundombinu si ajenda ya kisiasa pekee, bali ni sehemu ya kutafuta suluhisho la
changamoto zinazowakabili wananchi katika maisha na shughuli zao za kiuchumi.
Alisema hali mbaya ya
barabara katika baadhi ya maeneo imekuwa kikwazo kwa shughuli za uzalishaji,
usafirishaji wa bidhaa na upatikanaji wa masoko.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa
wa Mbeya, Beno
Malisa, alisema Mkoa
huo unatambua na kuthamini jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuboresha
miundombinu, hususan barabara.
Alisema Serikali imetenga
zaidi ya shilingi
bilioni 9 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya njia nne inayounganisha
Igawa–Uyole–Songwe–Tunduma,
akieleza kuwa mradi huo ni hatua muhimu katika kuboresha usafiri na
usafirishaji katika Mkoa wa Mbeya.
Kwa mujibu wa Mhe. Malisa,
ujenzi huo utasaidia kupunguza msongamano wa magari, kurahisisha usafirishaji
wa bidhaa na kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji.
“Mradi huu utarahisisha
usafiri na usafirishaji wa bidhaa, kupunguza msongamano wa magari na kufungua
fursa mpya za kiuchumi kwa wananchi na wawekezaji,” alisema.
Malisa alisema pamoja na
maboresho ya barabara, Serikali inaendelea kuwekeza katika huduma nyingine
muhimu, ikiwemo umeme na maji, ili kuweka mazingira bora kwa shughuli za
uzalishaji na uwekezaji.
Alisema TANESCO tayari imetoa
ratiba ya kupeleka umeme katika maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa wa huduma
hiyo.
Alibainisha kuwa upatikanaji
wa umeme katika maeneo ya uzalishaji, ikiwemo migodi inayozalisha hadi kilo 400 za dhahabu kwa
mwezi, utasaidia kuongeza tija na thamani ya uzalishaji.
Alisema maboresho ya huduma
za maji, umeme na miundombinu mingine yataendelea kuwa msingi muhimu wa
kuboresha maisha ya wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Mbeya.
Kwa ujumla, Serikali imeeleza kuwa uwekezaji
katika miundombinu utaendelea kupewa kipaumbele


No comments:
Post a Comment