Breaking News

May 6, 2025

MILA NA TAMADUNI ISIWE KIKWAZO KWA MTOTO WA KIKE KUPATA ELIMU


Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum,Dkt,Doroth Gwajima(picha  kwa msaada wa mitandao ya Kijamii)

MILA NA TAMADUNI ISIWE KIKWAZO KWA MTOTO WA KIKE KUPATA ELIMU

Na Hawa Mikidadi

Baadhi ya maeneo nchini Tanzania kumekuwa na mila na tamaduni ambazo zimekuwa kikwazo katika elimu hasa kwa watoto wa kike ambazo zinaleta athari chanya kwa jamii inayomzunguka  mtoto wa kike.

 Katika ziara ya  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk.Samia Suluhu Hassan      mikoa ya Lindi na Mtwara iliyofanyika septemba 26,2023 moja ya mambo yaliyomgusa ni pamoja na hali duni ya elimu kwa watoto wa kike na kuwataka wananchi wa mikoa ya kusini kuwaacha watoto wasome na kutilia mkazo watoto wa kike.

Licha ya kuwepo sababu nyingi zinazowasukuma wasichana kukatisha masomo katika mikoa ya kusini ,mila na desturi zimekuwa zikichangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa hali hiyo,utamaduni wa jamii kuwacheza ngoma wasichana wakiwa katika umri mdogo ni moja ya mambo yanayosababisha mimba kwa wanafunzi.

Aidha,ripoti ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha 2021-2022 inaonyesha uwepo wa idadi kubwa ya wanafunzi wanaokatisha masomo katika mikoa hiyo ya kusini mwa nchi, ya elimu msingi (BEST2023),inaonyesha jumla ya wanafunzi wa sekondari 5736 walikatisha masomo mkoani Mtwara na wanafunzi 4875 mkoani Lindi.

Rais Samia alitumia ziara hiyo kuwataka wananchi wa mikoa ya kusini kuwaacha watoto wa kike wasome ambao ndiyo wamekuwa waathirika wa kukatishwa masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo ndoa na mimba utotoni.

“Niwaombe sana waacheni wasichana wasome ,shule ile ya wasichana ni maalumu kwa wenye vipaji vya sayansi huko ndipo tutapata walimu ,madaktari na wataalamu mbalimbali “alisema.

Akizungumzia hilo mkurugenzi wa chama cha wanahabari wanawake Tanzania(Tamwa) Dk Rose Reuben,anasema kinachofanywa na Rais ni uwajibikaji wa wazi katika kuhakikisha serikali inamuondolea mwanamke utegemezi.

Mbali na kuondoa utegemezi kwa wanawake Dk Rose anasema hatua hizo zinazoendelea kuchukuliwa na Rais Samia ,zinalenga kumsaidia mtoto wa kike kupata elimu katika mazingira bora bila kukumbana na vikwazo.

Kwa upande mwingine ,Mkuu wa kitengo cha mawasiliano shirika la msichana Initiative Sara Beda,hivi karibuni alinukuliwa na vyombo vya habari akisema upo umuhimu kwa jamii kutumia fursa zinazotolewa na serikali katika kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu .

“Msichana Initiative tunapongeza jitihada zinazofanywa na serikali kumkomboa mtoto wa kike katika elimu ,kwa kuwa tunaamini kwamba ndiyo njia ya kumwezesha kutimiza ndoto zao.”anasema Sara Beda.

Viongozi na vyombo mbalimbali  wanatilia mkazo mila na tamaduni potofu zinazomnyima haki ya elimu mtoto wa kike zinaondolewa katika jamii, ambapo baadhi ya kampeni zilizoanzishwa ni kama Muache asome iliyosaidia jamii kuamka kupeleka mtoto wa kike shuleni badala ya kumuozesha katika umri mdogo.

Aidha, ripoti ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 inaonyesha mkoa wa Mtwara una jumla ya watu 1,634,947 kutoka 1,270,854 wa sensa  ya mwaka 2012 na  mkoani Lindi ina idadi ya watu 1,194,028 kutoka watu 864,652 sensa ya mwaka 2012.

Pia, katika hali ya kielimu mkoani Mtwara na Lindi  kumekuwepo tamaduni za kuozesha watoto wa kike na kutoipa kipaumbele  elimu ya mtoto wa kike ,uhamasishaji wa wazazi kuhusu elimu bado upo chini.

Kupitia mila na tamaduni za mikoa ya kusini kumekuwa na athari mbalimbali zinazotokana na tamaduni hizo ambazo moja kwa moja zinamuathiri mtoto wa kike ikiwepo ndoa na mimba za utotoni,kuhamasisha mapenzi ya mapema kwa kujijua washakuwa watu wazima .

Kwa mujibu wa sera elimu ya mwaka 2014 toleo la mwaka 2023 inasema wazazi na walezi ni wadau muhimu katika kuimarisha maendeleo ya elimu kwa wanafunzi ili kufanikisha hilo ushirikiano kati ya mzazi,mlezi,walimu na uongozi wa shule ni muhimu kufuatilia nidhamu maadili na mwenendo wa kitabia wa mtoto wake.

Kwa mujibu wa ilani ya chama cha mapinduzi ,serikali imeimarisha miundombinu ya shule za sekondari kwa kujenga shule 26 za sekondari za wasichana za kidato cha tano na sita katika mikoa 26 nchini ili kuhakikisha wanafunzi wa kike wanapata elimu bora.

Ilani ya chama cha mapinduzi pia imeongeza nafasi za wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi na hisabati katika shule za sekondari hususani watoto wa kike.

 Sanjari na kuboresha mbinu na mikakati ya utoaji wa elimu nje ya mfumo rasmi (MEMKWA)ili kuwawezesha waliokosa fursa au kupoteza sifa za kusoma katika mfumo rasmi kuweza kutimiza ndoto zao za kielimu na kuchangia ipasavyo katika ujenzi wa Taifa.

Vile vile, kuhahikisha mfumo mzima wa elimu unajengwa kwa umadhubuti na kuzingatia utamaduni,mila na desturi za kitanzania na kuimarisha masomo ya maadili ,uzalendo wa kitaifa na uraia kwa shule zote nchini.

No comments:

Post a Comment