Breaking News

Jan 6, 2021

MBUNGE HAWA AHAMASISHA JAMII UNAWAJI MIKONO



Mhe.Mbunge Viti Maalum (CCM),Hawa Mchafu, Mkoa wa Pwani.

MBUNGE HAWA AHAMASISHA JAMII UNAWAJI MIKONO

NA VICTOR MASANGU, PWANI

JAMII imetakiwa kuhakikisha kwamba, inajenga tabia ya kunawa mikono mara kwa mara kwa ajili ya kuepukana na magonjwa mbali mbali ya milipuko ikiwemo kuumwa na tumbo na badala yake wazingatie maelekezo ambayo yanatolewa na wataalamu wa afya ili kuupukana na  hali hiyo.

Kauli hiyo, imetolewa na Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Pwani, Hawa Mchafu, wakati alikuwa akizungumza na baadhi ya wananchi kuhusiana na masuala mbalimbali ya kimaendeleo pamoja na kujadili, namna ya kuweza kukabiliana na magonjwa ya mlipuko ambayo yamekuwa yakiwakumba baaadhi ya wananchi.

Mchafu alisema kwamba, kwa sasa nia ya serikali ya awamu ya tano ni kuboresha huduma ya afya katika maeneo mbali mbali ikiwemo Zahanati, vituo vya afya, pamoja na hospitali ili kuweza kuwapatia huduma iliyo bora  kwa wananchi sambamba na kuhakikisha kwamba, wanahudumiwa bila ya kupata usumbufu wowote.

“Kikubwa ninachowaomba wananchi, pamoja na jamii kwa ujumla, ni lazima tubadilike kwa kuhakikisha kwamba, tunakuwa na utaratibu wa kunawa mikono yetu katika vipindi tofauti, na tukifanya hivi nina imani kubwa tutaweza kabisa kuepukana na magonjwa mbalimbali ya milipuko ambayo imekuwa ikijitokeza katika maeneo ambayo tunaishi, hivyo ni vema tukazingatia mwongozo unaokuwa ukitolewa na wataalamu wetu wa afya,”alisema Hawa.

Kadhalika, aliongeza kuwa, ni lazima pia wananchi wawe na utaratibu wa kusafisha maeneo yao mbalimbali ambayo wanaishi pamoja na kufyeka nyasi na kufikia madimbwi ya maji, ambayo ndio yamekuwa ni chanzo kikubwa na kusababisha kutokea kwa magonjwa mbalimbali ya milipuko ikiwemo ugonjwa wa kipindupindu.

Aidha, Mbunge huyo, aliahidi kuendelea kushirikiana na wananchi, pamoja na wataalamu wa afya katika kuweka mipango madhubuti ya kutoa elimu ya mara kwa mara, hasa katika maeneo ya vijijini ili kuweza kutoa elimu ambayo itaweza kuwa ni moja ya msaada na mkombozi mkubwa wa kuwasaidia wananchi kujikinga na magonjwa ya mlipuko.

Nao, baadhi ya wananchi Wilayani Kibaha, wamempongeza Mbunge huyo, kwa kuweza kuwatembelea katika maneo yao na kuwapa elimu inayohusiana na magonjwa ya mlipuko na kwamba maelekezo hayo watayafanyia kazi ili kuweza kuondokana kabisa na hali hiyo ya kuumwa magonjwa  hayo na kwamba wameiomba serikali ya awamu ya tano, kuwaboreshea huduma zaidi ya matibabu katika maeneo ya vijijini.

 


No comments:

Post a Comment