Breaking News

Apr 6, 2025

CWT MOROGORO WALIRIDHISHWA NA UTENDAJI KAZI WA RAIS SAMIA

 

Mwenyekiti CWT Mkoa wa Morogoro,Jumanne Nyakirang'ani


Chama cha Walimu Morogoro waliridhishwa na utendaji kazi wa Rais Samia

Na Thadei Hafigwa

WALIMU wa Wilaya ya Morogoro yenye halmashauri mbili,Morogoro mjini na vijijini mwishoni mwa wiki walifanya mkutano mkuu ulioenda sambamba na uchaguzi wa viongozi wa ngazi mbalimbali katika chama cha walimu Tanzania Wilayani humo.

Katika mkutano huo ulihudhuriwa na wawakilishi wa wafanyakazi sehemu za kazi ambao mchakato wake ulizingatia demokrasia,kwamba wajumbe hao ni ngazi ya kwanza ya utetezi,pia ni kiungo muhimu cha mawasiliano kati ya wilaya na wafanyakazi wenzao.

Wajumbe walipitia taarifa za utendaji wa kazi ya miaka mitano pamoja na mapato na matumizi,sanjari na kuwachagua viongozi wa chama wao katika nafasi ya Mwenyekiti,mwekahazi na wajumbe wa kamati tendaji.

Miongoni mwa viongozi walioshiriki katika mkutano huo ni Mwenyekiti wa chama cha walimu Mkoa wa Morogoro,Jumanne Nyakirang’ani ambaye alielezea changamoto mbalimbali zinazowakabili walimu waliopo katika halmashauri ya Wilaya ya Morogoro na manispaa ya Morogoro.

Nyakirang’ani alionesha kuridhishwa kwake na uamuzi wa serikali kwa kufungua madaraja ya walimu sambamba na kubadilisha muundo wa utumishi.

Aidha,miongoni mwa watendaji wa kazi wa serikali ni pamoja na Maafisa utumishi na ofisi ya TSC Wilaya ambao walishughulikia suala la marejesho kwa kuwa katika wilaya hiyo changamoto ya kusahaulika walimu katika upandaji vyeo ni ndogo ukilinganisha na wilaya nyingine.

Mkurugenzi mtendaji,Halmashauri ya Morogoro,Jeshi Lupembe

”chama chetu kimepiga hatua kubwa katika jitihada za kutetea haki na masilahi ya walimu ikiwa pamoja na kutoa elimu kwa wanachama na kuwajengea uwezo wa kudahi haki zao.”alisema

Katika Mkutano huo,walimu wa wilaya ya Morogoro walianisha mafanikio ambayo wameshughulikiwa na serikali na serikali ya awamu ya sita kwa kupandishwa madaraja walimu wapatao 999 katika wilaya ya Morogoro sawa na asilimia 54 ya walimu wote wa wilaya ya Morogoro vijijini.

Serikali imetoa ruzuku ya fedha ya likizo mara mbili kila mwaka hivyo walimu wanakwenda likizo japo fedha zinazotolewa katika wilaya hiyo hazichosherezi idadi ya walimu waliopo.

Katibu wa Chama Cha walimu,manispaa ya Morogoro,George Lukoa

Walibainisha pia katika kipindi cha miaka miwili serikali imeweza kuajiri walimu 208 ili kukabiliana na upungufu wa walimu ikiwa ni mkakati wa kuongeza ufaulu kwa wanafunzi,pamoja na kulipwa kwa walimu 235 waliokuwa wanadai malimbikizo ya mishahara kwa mwaka 2024. 

John Kigongo ni katibu wa chama cha walimu Morogoro vijijini alisema kuwa pamoja na mafanikio yao lakini alishauri serikali ikielekeze katika ujenzi wa nyumba bora za walimu kama walivyoweza kufanikisha ujenzi wa madarasa ya kisasa.

Kigongo alisema kuwa walimu wakiwa katika mazingira bora ya kuishi inawaongezea ari ya kufanyakazi kwa kuwa iwapo inachangia ufaulu wa wanafunzi.

Katibu wa CWT Morogoro vijijini,John Kigongo kushoto,akiwa na mwenyekiti wake Mbarouk Chipeta akifuatilia kwa karibu hoja za uboreshaji na utendaji kazi wa Chama hicho.

Hata hivyo,changamoto zinazowakabili walimu ni pamoja na madeni ya uhamisho ya kuanzia mwaka2017 hadi sasa hasa katika idara ya elimu ya msingi walimu 218,na kwa upande wa walimu wa shule za sekondari ni walimu 106.

Kadhalika yanayotokana na malimbikizo ya mishahara tangu mwaka 2014 hadi sasa walimu 621 wanadai bila ya mafanikio na madai yao kutopandishwa katika mfumo japo wamejaza fomu za maombi ya malipo zaidi ya mara moja.

Kwa upande wake,Jeshi Lupembe ni Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Morogoro alikiri kutambua changamoto zinazowakabili walimu na kwamba ofisi yake ipo tayari kuzifanyia kazi kwa kuwa mchango wa walimu hapa nchini ni mkubwa.

Lupembe alisema kuwa suala ya haki za wafanyakazi ikiwemo walimu zinapaswa kulindwa na kusimamiwa kikamilifu.pamoja na changamoto walizonazo walimu wanapaswa kujiongeza kwa kufanya shughuli za kujiongezea kipato siku za mapumziko,jumamosi na jumapili.

Musa Kilakala ni mkuu wa Wilaya ya Morogoro amewahakikishia walimu kwamba changamoto walizonazo zitafanyiwa kazi kwa kuitisha kikao kazi kitakachowakutanisha wakurugenzi wa halmashauri mbili,halmashauri ya Morogoro vijijini na Manispaa ya Morogoro,maafisa utumishi na idara ya fedha ili changamoto za walimu zipatiwe ufumbuzi.

Kilakala aliwakumbusha walimu kutumia chama chao (CWT) ambacho serikali inakitambua.hivyo waendelee kuwa wamoja na kushikamana katika kutumiza wajibu wao kama ilivyo kaulimbinu yao,wajibu na kazi.

George Lukoa katibu wa CWT manispaa ya Morogoro alionesha kuridhishwa na maelekezo ya Mkuu wa Wilaya Musa Kilakala katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili walimu.

Lukoa alisema kuwa ofisi yake itaendelea kuwahudumia walimu na kuwahimiza wanatekeleza wajibu wao wakati serikali ikiendelea kuzipatia majawabu.

No comments:

Post a Comment