Breaking News

Sep 11, 2020

SEKTA YA USTAWI WA JAMII NI NYEZO YA KUFIKIA UCHUMI WA JUU

Na Andrew Chimesela – Morogoro


Imeelezwa kuwa sekta ya Ustawi wa Jamii hapa nchini inayotekelezwa na Maafisa wa Ustawi wa Jamii chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto ni nyezo muhimu  na chimbuko la kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa juu.

Hayo yamelezwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Kalobelo Agosti 27 mwaka huu wakati akifungua kikao cha wadau wanaotoa huduma za Ukimwi na watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi Mkoani Morogoro.

Katika kikao hicho kilichofanyika Ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na kujumuisha Maafisa wa Ustawi wa Jamii, Mhandisi kalobelo amesema Tanzania inapojipanga kuelekea uchumi wa juu umuhimu wa Maafisa hao unazidi kutambulika na kwamba maafisa hao hawawezi kujiondoa kama sehemu ya kuipeleka nchi katika ustawi wa juu zaidi.

Amesema kwa sababu hiyo Maafisa Ustawi wa Jamii wajiamini na kwamba hata hatua ya Tanzania ilipofikia sasa kwa sehemu kubwa wao wamechangia kwa kuziwezesha familia na jamii kwa jumla kuishi kwa Amani na utulivu.

“na huenda hata tulipofikia katika uchumi wa kati pia nyie mmekuwa wadau muhimu katika kutufikisha hapo” amesema Mhandisi Kalobelo.

Amesema sehemu yoyote yenye migogoro haiwezi kuwa na maendeleo ya haraka, hivyo amewataka maafisa Ustwai wa Jamii kufanya kazi kwa bidii katika kuleta utulivu ndani ya nchi ili jamii ipate fursa ya kufanya kazi ya kujiletea maendeleo yao.

Aidha, ametumia fursa hiyo kuwashukuru wahisani wanaosaidia masuala ya huduma za Ustawi wa Jamii hususan eneo la kuhudumia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

 

Pamoja na kuwashukuru wahisani hao ambao wamewezesha kutekelezwa kwa afua mbalimbali kwenye eneo la watoto katika ngazi ya jamii, amewataka wahisani hao kufanya kazi zao kwa uaminifu ili kile kinachoombwa kwa ajili ya kuwasaidia watoto kiwafikie ili watoto hao nao wafaidi rasilimali za nchi yao.

Mwisho, amewataka wale wote wenye vituo vinavyojihusisha na utoaji wa huduma kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu, kusajili vituo vyao ili pamoja na nia yao njema ya kusaidia watoto hao vituo hivyo vifuate taratibu za nchi na kutambulika kisheria.

Naye Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Morogoro Bi. Jesca Kagunila alitaja lengo kuu la kikao hicho kuwa pamoja na kufahamiana mashirika yote yanayojihusisha na kutoa huduma kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, kikao hicho kililenga kuboresha utendaji kazi na namna ya kutatua changamoto za Matukio ya Ukatili kwa watoto ndani ya Mkoa wa Morogoro.

Aidha, Bi kagunila amesema kuanzia mwezi Januari hadi Juni mwaka huu jumla ya matukio 2848 ya ukatili yariripotiwa, kati yake matukio 1561 walifanyiwa watu wazima na matukio ya ukatili 1287 walifanyiwa watoto.

Katika matukio yote hayo ukatili wa kihisia umeonekana kuongoza kwa kuripotiwa matukio 1287 na kufuatiwa na ukatili wa kimwili matukio 699, ukatili wa kiuchumi matukio 551 na ukatili wa kingono matukio 111 huku Halmashauri ya Mji wa Ifakara ikiongoza kwa kuripoti matukio ya ukatili 1873.

Akifunga kikao hicho kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa, ambaye baada ya kufungua alipata dharura, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Urio Kusirye ametaka kuimarisha ushirikiano kwa wadau wanaofanya kazi za kuhudumia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi na kuagiza ngazi za Wilaya nao kuitisha vikao kama hivyo.

Wadau mbalimbali akiwemo Christina Wirner wa kutoka kituo cha Agape Chidren’s cha Kihonda Mkoani humo ameiomba Serikali kuendelea kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote wanaojihusisha na ukatili kwa watoto hasa katika eneo la Ubakaji na kulawiti ili jamii igope kufanya matendo kama hayo.

Naye Mkuu wa Dawati la Jinsia na watoto – Polisi Mkoa wa Morogoro Sophia Ngosso amesema changamoto kubwa wanayoipata jeshi la polisi katika suala la ukatili kwa watoto ni jamii kutokuwa tayari kutoa ushahidi pindi wahusika wanapohitajika.

 

Kwa sababu hiyo watuhumiwa huachiwa na ndipo dhana iliyojengeka miongoni mwa jamii kuwa polisi inawaachia watuhumiwa huanzia. Kwa sababu hiyo Sophia ameiomba Jamii pamoja na kuripoti matukio hayo jamii iwe tayari kutoa ushirikiano katika kutoa ushahidi ili kuwatia hatiani watuhumiwa na kukomesha matendo ya ukatili kwa watoto.

Wadau wa kikao hicho akiwemo Bi Ruth Mnale kutoka kituo cha Day Care Centre amewatuhumu baadhi ya wazazi kutetea ukatili wa kingono wanaofanyia watoto wao ambapo hudai kuwa watoto hao nao wanahitaji starehe kama watu wazima.

Naye Peter Kimath kutoka kituo cha kutoa msaada wa kisheria ameishukuru Serikali kwa kutoa ushirikiano kwao mara wanapokuwa wanahitaji hususan jeshi la polisi.

No comments:

Post a Comment