Breaking News

Aug 29, 2026

ELIMU YA MAFUTA NA GESI ASILIA YAWAVUTIA WANANCHI MOROGORO

 

 ELIMU YA MAFUTA NA GESI ASILIA YAWAVUTIA WANANCHI MOROGORO

 Na Thadei Hafigwa

WANANCHI waliofika kutembelea banda la Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) katika Tamasha la Nne la Taifa la Utamaduni mkoani Morogoro wameonyesha shauku kubwa ya kupata elimu kuhusu shughuli za utafutaji, uchimbaji na uendelezaji wa rasilimali za mafuta na gesi asilia nchini.

Shauku hiyo ilijitokeza baada ya wananchi mbalimbali kufika katika banda hilo na kuuliza maswali kuhusu uwepo wa mafuta nchini, hatua zilizofikiwa katika utafutaji wa rasilimali hiyo pamoja na lini Tanzania inaweza kuanza kunufaika na uchimbaji wa mafuta.


Baadhi ya wananchi hao,ni Charles Pangapanga,Mkulima wa skimu ya Umwagiliaji Mvomero abaye alihoji iwapo tayari kuna uhakika wa uwepo wa mafuta nchini na ni lini shughuli rasmi za uchimbaji zinaweza kuanza.

Mjiolojia kutoka PURA, Lukelo Matimbwi, alisema kuwa bado kuna tafiti na shughuli za utafutaji zinazoendelea katika maeneo mbalimbali nchini ili kubaini uwepo na kiwango cha rasilimali za mafuta.

Alisema kuwa hadi sasa, Tanzania imefanikiwa kubaini uwepo wa gesi asilia, huku uchunguzi na tafiti za kutafuta mafuta zikiendelea kwa mujibu wa taratibu na teknolojia zinazotumika katika sekta ya petroli.

Matimbwi alieleza kuwa elimu inayotolewa na PURA inalenga kuwawezesha wananchi kuelewa nafasi ya mamlaka hiyo katika kusimamia na kudhibiti shughuli za mkondo wa juu wa petroli, zikiwemo shughuli za utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi asilia.

Aidha, wananchi waliofika katika banda hilo walipata fursa ya kuuliza maswali na kujifunza zaidi kuhusu rasilimali za mafuta na gesi asilia pamoja na mchango wake unaotarajiwa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

Tamasha la Nne la Taifa la Utamaduni, linaloendelea katika Viwanja vya Jamhuri mkoani Morogoro, limeendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi mbalimbali za serikali na wadau wengine kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu, huduma na fursa zinazopatikana katika sekta mbalimbali.

Kwa upande wake,Chifu wa Morogoro,Musa Lukwele amezipongeza Taasisi za serikali ambazo zimeshiriki katika Tamasha la Utamaduni limefanya uamuzi wa kizalendo,na kutoa elimu huduma wanazotoa kwa wananchi,na tafiti mbalimbali zinazofanywa na wataalamu katika kuharakisha maendeleo ya nchi.

Chifu Lukwele,alisema kuwa Machifu na Wazee wa Mila,pamoja na majukumu yao mengine wataendelea kutoa ushirikiano kwa serikali na watafiti watakapofika maeneo yao ya kiutawala ili kusipatwe vikwazo katika majukumu yao ya kuwaletea maendeleo yao.

No comments:

Post a Comment