Breaking News

Jul 27, 2025

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

 NAIBU KATIBU MKUU WA WIZARA YA ELIMU,SAYANSI NA TEKNOLOJIA,DK.HUSSEIN OMARY AKISISITIZA JAMBO.

RAIS SAMIA APONGEZWA UWEKEZAJI KWA WALIMU KATIKA TEHAMA

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

WALIMU zaidi 5000 wa shule za sekondari hapa nchini kutoka kanda 7 wamenufaika na mafunzo ya  TEHAMA katika kipindi cha miaka mitatu, ambapo kwa mwaka huu pekee, walimu 1,870 wameshiriki mafunzo hayo yaliyofanyika katika vituo vya Tukuyu - Mbeya na Chuo cha Ualimu Morogoro kutokana na uwekezaji uliofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk.Samia Suluhu Hassan

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward Wawa alibanisha hayo katika mjini Morogoro katika hafla ya kufunga mafunzo ya awamu ya tatu kwa walimu kutoka mikoa ya Morogoro,Pwani,Dar es Saalam,Lindi na Mtwara.

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Edward akiwasilisha taarifa yake kwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia,Dk.Hussein Omary.

Wawa alisema kuwa kuwa serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeanza kutekeleza mradi wa kuboresha elimu ya sekondari kwa kuimarisha ujuzi wa walimu kupitia mafunzo ya TEHAMA  toka mwaka 2022 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kiashiria na 9 cha mradi wa matokeo makubwa kinacholenga kuwajengea walimu uwezo wa kufundisha kwa kutumia mbinu za kisasa na vifaa vya kidijitali.

Mafunzo hayo yametekelezwa kwa awamu tatu,kwa kuzingatia kanda 7 zilizopo,katika awamu ya kwanza,iliyofanyika mwaka 2022/2023,walimu 500 kutoka kanda ya kati na kanda ya kaskazini,walipatiwa mafunzo hayo.

“Awamu ya pili yalifanyika mwaka 2023/2024 ambapo walimu 2632 kutoka kanda ya Ziwa,kanda ya magharibi,kanda ya kaskazini na kanda ya kati,walipatiwa mafunzo”alisema.

Baadhi ya Walimu Washiriki wa mafunzo ya Tehama mjini Morogoro walifuatilia kwa umakini Hotuba ya Mgeni Rasmi,Naibu Katibu Mkuu,Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Dk.Hussein Omary (hayupo pichani) kwenye hafla ya kufunga mafunzo hayo yaliofanyika katika Chuo cha Ualimu,Morogoro.

Aidha,alifafanua kuwa awamu ya tatu ya mafunzo kwa walimu wa Tehama yamefanyika katika mwaka 2024/2025 kwa kuhusisha vituo viwili,kituo cha kwanza Tukuyu Mbeya yalianza Julai 14-18,2025 na kuwanufaisha walimu 941,na Morogoroo ambapo jumla ya walimu 929 wamenufaika na mafunzo hayo.

Mgeni Rasmi wa hafla hiyo ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Hussein Omary, ambapo ametoa wito kwa walimu nchini kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo ya kitaaluma kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, akisisitiza kuwa elimu jumuishi na yenye usawa ni msingi wa maendeleo endelevu ya taifa.

Dk. Hussein alisema kuwa serikali ina dhamira ya dhati ya kuwekeza kwa walimu ili kuimarisha elimu bora inayomfikia kila mtoto, bila kujali mahali alipo,wizara yake inaendelea kutekeleza sera ya elimu kwa vitendo, kwa kuweka mkazo katika mitaala, miundombinu, TEHAMA na maendeleo ya walimu ili kuhakikisha maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Sami Suluhu Hassan yanatimia.

“Mafunzo haya ni tafsiri ya maono ya Mheshimiwa Rais. Tunatekeleza kwa vitendo sera ya elimu jumuishi na bora. Lengo ni kuhakikisha kila mtoto anapata elimu sawa,bila kujali eneo analotoka,” alieleza.

Dk. Hussein alisisitiza nafasi ya walimu kama nguzo kuu ya mabadiliko katika mfumo wa elimu nchini, akisema mafanikio ya elimu hayawezi kupatikana bila uwekezaji wa kweli kwa walimu.

Baadhi ya washiriki wa hafla ya kufunga mafunzo kwa walimu wa sekondari juu ya TEHAMA,Mjini Morogoro

Aidha, alibainisha kuwa serikali imeanza kuimarisha miundombinu ya kufundishia kwa kutumia TEHAMA ili kukabiliana na changamoto za karne ya 21, huku akiwataka walimu kuwa mfano kwa jamii kwa kuonyesha weledi, maadili na ubunifu katika kazi zao.

Mafunzo hayo yamewahusisha walimu kutoka shule mbalimbali nchini yakiwa na malengo kuwajengea uwezo kwa kutumia vifaa na rasilimali za Tehama  darasani,kuongeza ubora wa utoaji wa elimu kupitia mbinu shirikishi za kidigitali,kuimarisha matokeo ya ufundishaji kwa wanafunzi kupitia teknolojia.

No comments:

Post a Comment