Breaking News

Jun 22, 2025

Serikali Yapongeza CAMFED Tanzania kwa Uwekezaji Madhubuti katika Maendeleo ya Wasichana

 Bi. Rhoda Sheba, Afisa Elimu wa Watu Wazima, Elimu Nje ya Mfumo Rasmi na Elimu Maalum,Mkoa wa Morogoro.

Serikali Yapongeza CAMFED Tanzania kwa Uwekezaji Madhubuti katika Maendeleo ya Wasichana

Na Thadei Hafigwa, Morogoro

Serikali kupitia Ofisi ya Elimu Mkoa wa Morogoro imepongeza Shirika la CAMFED Tanzania kwa mchango mkubwa katika kuwawezesha wasichana kielimu, kijamii na kiuchumi—juhudi zinazotajwa kuwa nguzo muhimu katika ustawi wa taifa.

Pongezi hizo zilitolewa kupitia hotuba ya Afisa Elimu wa Mkoa wa Morogoro, iliyosomwa kwa niaba yake na Bi. Rhoda Sheba, Afisa Elimu wa Watu Wazima, Elimu Nje ya Mfumo Rasmi na Elimu Maalum,Mkoa wa Morogoro wakati wa ufunguzi wa Kongamano la  mafunzo maalum kwa wasichana waliomaliza sekondari na kufadhiliwa na CAMFED,iliyojumuisha Wilaya za Iringa,KILOLO,Chamiwino,Morogoro vijijini,Mlimba ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kujiunga na vyuo vya kati na vyuo vikuu.

“CAMFED siyo tu inatoa ufadhili wa masomo, bali inajenga mfumo wa ufuatiliaji wa maendeleo ya kielimu na maisha ya baadaye ya wanufaika wake. Huu ni mfano wa kuigwa katika kujenga kizazi imara cha wasomi na viongozi wa kesho,” alisema Bi. Sheba.

Aliongeza kuwa amewahi kushuhudia mnufaika wa CAMFED aliyekuwa likizo kutoka chuo kikuu akijitolea kuwahamasisha na kuwaelekeza wasichana walioko sekondari—ishara ya ushawishi chanya wa mpango huo katika kuendeleza mnyororo wa mafanikio.

Takwimu za mwaka 2024 zinaonesha kuwa CAMFED Tanzania imefadhili zaidi ya wasichana 154,201, na idadi hiyo imeokwenda sambamba na ngezeko la ufaulu katika mitihani yao ya kidato cha nne katika elimu ya sekondari, hatua iliyopokelewa kwa shangwe na pongezi kutoka kwa washiriki wa Kongamano hilo.

“Ni jambo la kujivunia kuona idadi kubwa ya watoto wa kike wakifanikiwa licha ya changamoto lukuki zinazowakabili. Mafanikio haya yanaonesha wazi kuwa uwekezaji kwa mtoto wa kike ni uwekezaji wenye tija kwa taifa,” aliongeza Bi. Sheba.

Washiriki wa Kongamano la Mafunzo maalum kwa Wanachuo tarajali,lilikofanyika katika shule ya Sekondari ya Kilakala,Morogoro wakifuatilia kwa umakini hotuba ya Mgeni Rasmi.

Mafunzo na Uwezeshaji wa Viongozi wa Baadaye

Mbali na ufadhili wa masomo, CAMFED Tanzania inatekeleza programu mbalimbali za kuwajengea uwezo wasichana katika uongozi, ujasiriamali, na stadi za maisha kupitia kwenye shule za sekondari.

Akizungumza katika Kongamano hilo la mafunzo, Mkuu wa Idara ya Miradi wa CAMFED Tanzania, Bi. Dominica Lyambo, alibaisha program ya kuwajengea uwezo wasichana uwezo kuelekea kujiunga na vyuo ni shule ya sekondari Kilakala (Morogoro), Ng’anza (Mwanza), na Shule ya wasichana ya Mkoa wa Pwani.

Lyambo alisema shirika hilo linafanya kazi katika nchi tano za Afrika ambazo ni Tanzania, Zambia, Zimbabwe, Ghana, na Malawi.

Mkuu wa Idara ya Miradi wa CAMFED Tanzania, Bi. Dominica Lyambo akiwasilisha taarifa yake,Mjini Morogoro katika Kongamano la wasichana ambao ni wanachuo tarajali wanaofadhiliwa na shirika lake

“Tanzania tulianza mwaka 2005 na tumesajiliwa rasmi mwaka 2006. Kwa sasa tunafanya kazi katika mikoa 10 na halmashauri 35, huku lengo la mwaka 2025 likiwa ni kufikia halmashauri 41,” alisema Bi. Lyambo.

Aliongeza kuwa CAMFED tayari imefikia halmashauri zote katika mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro, na kazi inaendelea katika mikoa mingine ili kufanikisha lengo la kufikia halmashauri zote 76 zilizopo kwenye mikoa hiyo 10.

Uwajibikaji na Ulinzi wa Mtoto

Kwa mujibu wa Bi. Lyambo, utekelezaji wa miradi ya CAMFED unazingatia misingi ya utawala bora, ikiwemo sera ya ulinzi wa mtoto, usimamizi wa rasilimali, na uwajibikaji wa kifedha. Aidha, shirika hilo linafanya kazi kwa karibu na wadau kutoka ngazi ya kijiji hadi wizara, wakiwemo maafisa ustawi wa jamii, kamati za shule, na maafisa elimu kata.

“Tunaamini mtoto wa kike akipewa mazingira salama ya kusoma, akiheshimiwa na kuthaminiwa, ana nafasi kubwa ya kufikia ndoto zake na kuondokana na umaskini,” alieleza.

Bi. Lyambo pia alibainisha kuwa mafanikio ya CAMFED yametokana na ushirikiano mzuri na wanachama wa CAMFED Association—ambao ni wanufaika waliorejea kuleta mabadiliko katika jamii zao.

Sauti za Wanufaika

Mmoja wa wanufaika wa mpango huo, Salma Salum, alieleza kuwa CAMFED imekuwa msaada mkubwa katika maisha yake kwa kumwezesha kielimu na kumwandaa kiakili na kisaikolojia kwa safari ya elimu ya juu.

“Ninaishukuru CAMFED kwa kutuwezesha siyo tu kielimu, bali pia kwa kutujengea uwezo wa kukabiliana na changamoto tunazokutana nazo tunapoingia vyuoni,” alisema.

Je, Wavulana Watasahaulika?

 CAMFED ilifafanua kuwa kwa sasa mpango huo umejikita kwa wasichana kutokana na changamoto maalum wanazokumbana nazo, lakini mjadala huo umefungua fursa ya kutafakari upanuzi wa wigo wa mnufaika katika siku zijazo.

No comments:

Post a Comment